SOPHIA Mjema, Mkuu wa Wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam, amepiga marufuku mikusanyiko ya watu katika baa, ikiwa ni sehemu ya hatua za kudhibiti maambukizi ya Ugonjwa wa Homa Kali ya Mapafu inayosababishwa na Virusi vya Corona (COVID-19). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Mjema ametoa marufuku hiyo jana tarehe 17 Aprili 2020, na kuelekeza wamiliki wa baa hizo kuhakikisha wateja wao wanaonunua bia, wanakwenda kunywea nyumbani.
Mjema amesema mtu yeyote atakaye kiuka agizo hilo atachukuliwa hatua za kisheria.
“Waendesha baa mnaelekezwa kuwa vinywaji vitauzwa na mnunuzi atapaswa kunywea nyumbani, na sio kwenye baa. Ni wajibu wa kila mmoja kuzingatia maelekezo haya kwani hatua za kisheria zitachukuliwa kwa mmiliki, muendeshaji na mtu yeyote atakaye onekana kwenye eneo la baa akiendelea kunywa,” amesema Mjema.
Jiji la Dar es Salaam linaongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya maambukizi ya COVID-19, ikifuatiwa na Zanzibar.
Kwa mujibu wa taarifa ya Ummy Mwalimu, Waziri wa Afya, jiji hilo lina wagonjwa wapya 38 kati ya wagonjwa 53 walioripotiwa jana katika mikoa saba.
Leave a comment