SERIKALI imeingiza zaidi ya Sh. 7 Bilioni kutokana na malipo ya hati mpya za kusafiria na vibali vya ukaazi kwa njia ya kielektroniki (E-Visa & E-Permit). Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Hayo amesema Kamishna Mkuu wa Idara ya Uhamiaji, Dk. Anna Makakala uzinduzi wa hati za kusafiria na vibali vya ukaazi kwa njia ya kielektroniki (E-VISA & E-PERMIT).
Dk. Makakala amesema katika kipindi cha mwaka wa fedha wa 2017/18 vibali vya ukaazi 18,008 vilitolewa kwa wageni. Vile vile, kuanzia mwezi mwishoni mwa Januari hadi Novemba 25, 2018 jumla ya hati mpya za kusafiria za kielektroniki 55,177 zimetolewa.
“Zaidi ya shilingi bilioni 7 zimepatikana kutokana na malipo ya hati mpya za kusafiria za kielektroniki. Katika kipindi cha mwaka wa fedha 2017/2018 vibali vya ukaazi 18,008 vilitolewa kwa wageni ,kuanzia Januari 31, 2018 hadi Novemba 25, 2018 jumla ya hati mpya za kusafiria za kielektroniki 55,177 zimetolewa,” amesema Dk. Makakala.
Dk. Makakala amesema ifikapo mwezi Januari mwaka 2019 huduma ya upatikanaji wa hati mpya za kusafiria za kielektroniki itakuwa imesogezwa katika balozi zote za Tanzania ili kuwarahisishia Watanzania walioko nje ya nchi kupata hati hizo.
Akizungumzia kuhusu mfumo huo, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Augustine Mahiga amesema mfumo huo mpya utarahisisha Tanzania kupata wawekezaji wengi na kuagiza utaratibu wa ukaguzi wa wageni wanaoingia nchini hasa watalii ufanyike kwa njia rafiki ili kuondoa malalamiko.
Naye Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Mohammed Aboud amesema mfumo huo utawezesha ukuzaji wa sekta za uchumi ikiwemo uwekezaji na utalii na kuongeza pato la taifana ajira kwa vijana.
Leave a comment