MWANAHABARI Erick Kabendera, anayekabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, amefanyiwa vipimo vya X-Ray na damu katika Hospitali ya Rufaa ya Amana. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Leo tarehe 18 Septemba 2019, mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi Augustine Rwizile, Kabendera amedai kuwa, jana tarehe 17 Septemba 2019 kwa mara ya kwanza, amefanyiwa vipimo hivyo na kubainika kwamba ana matatizo ya mgongo.
Kabendera amedai kuwa, amechukuliwa vipimo vingine ambavyo matokeo yake yanaweza kuwa tayari mwishoni mwa wiki hii, huku akieleza kwamba anapata maumivu makali ya mgongo.
Baada ya kueleza hayo, upande wa jamhuri kupitia Wakili wa Serikali, Wankyo Simon, uliieleza mahakama hiyo kwamba upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika, lakini upo kwenye hatua za nzuri.
Hakimu Rwizile ameahirisha kesi hiyo hadi Oktoba Mosi mwaka huu.
Awali, tarehe 12 Septemba 2019 mahakama hiyo iliombwa kulielekeza Jeshi la Magereza kuruhusu Kabendera kupata matibabu, kutokana na afya yake kuzidi kuzorota.
Mbele ya Hakimu Rwizile, Wakili wa Kabendera, Jebra Kambole alidai, hali ya mwanahabari huyo ni tete kiasi kwamba mguu wake wa kulia unashindwa kutembea kutokana na kupooza, pia kupata shida ya kupumua nyakati za usiku.
Pia, Wakili Kambole aliiomba mahakama hiyo kulielekeza Jeshi la Magereza kutoa taarifa rasmi ya ugonjwa unaomsumbua Kabendera.
Kabendera aliieleza mahakama hiyo kuwa, anapata maumivu makali ya paja na mfupa wa mguu wa kulia, na kwamba alipimwa damu na kuchomwa sindano tatu zilizosaidia kupoteza tatizo kwa muda.
Kabendera anakabiliwa na mashtaka matatu ikiwemo madai ya kujihusisha na genge la uhalifu, kukwepa kodi kiasi cha Sh. 173,247,047.02 na utakatishaji fedha.
Leave a comment