BAADHI ya wajumbe na wanachama wa Chama cha Wafugaji Tanzania (CCWT) wameendelea kuvutana na uongozi wa juu chama hicho wakitaka viongozi kuachia madaraka na kufanyika uchaguzi, anaandika Dany Tibason.
Baadhi ya madai ya wanachama na wajumbe wa chama hicho kutaka viongozi kuachia ngazi ni pamoja na kudaiwa kushindwa kutimiza majukumu yao ikiwa ni pamoja na kushindwa kuitisha mkutano wa kusoma mapato na matumizi.
Hoja nyingine ni pamoja na kudai kwamba viongozi hao wanafanya ujanja wa kubadili kadi za uanachama wa chama hicho ikiwa ni pamoja na kubadili nembo ya awali ya chama hicho.
Mmoja wa Wenyeviti hao,Wamarwa Kusundwa alisema kuwa waliuchagua uongozi wa mpito ambao ni mwenyekiti, katibu mkuu, mtunza hazina pamoja na wajumbe 12 wa kamati tendaji mnamo mwaka 2015 kwa lengo la kutetea maslahi ya wafugaji.
“Kwa kweli tunashindwa kuuelewa uongozi huu wa sasa kwa sababu umekuwa ukijifanyia mambo kivyake bila kushirikisha kamati tendaji wala bodi ya wadhamini na mbaya zaidi hawajawahi kusoma mapato na matumizi tangu wachaguliwe,”alisema.
Katibu wa Chama cha Wafugaji nchini, Magambe Makoye hakuwa tayari kuzungumzia sakata hilo alipotakiwa kutoa ufafanuzi.
Leave a comment