SERIKALI imewataka viongozi wa dini kuacha kujiingiza kwenye siasa badala yake waendelee kuimarisha amani na mshikamano kwa jamii, anaandika Mwandishi Wetu.
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo, amesema hayo alipokuwa akifungua kikao cha pamoja kati ya viongozi wa madhehebu ya dini na serikali.
Amesema viongozi wa dini wana jukumu la kuendelea kuimarisha mshikamano kwa kuhubiri amani hivyo wasijiingize kwenye siasa kwa kuwa siyo sehemu ya kazi zao.
Aliongeza kuwa atawashangaa iwapo viongozi wa dini wataanza kujiingiza kwenye siasa na kuvipigia debe vyama vya kisiasa huku wakisahau jukumu lao la kuongoza roho za watu wa dini hizo, kwani ipo siku watajikuta hakuna waumini na nchi itaangamia.
Gambo alisema serikali ya mkoa imeweka mkakati wa kuwashirikisha viongozi wa dini kwenye maandalizi ya bajeti na kuwapatia taarifa mara baada ya bajeti kuwasilishwa kwenye ngazi husika.
Aidha, amesema kikao hicho ni cha kwanza cha viongozi wa serikali na madhehebu yote ya dini kufanyika na akamuagiza Katibu Tawala wa Mkoa kuandaa ratiba ya kukutana na viongozi wa dini angalau mara mbili kwa mwaka ili kuangalia changamoto mbalimbali.
Leave a comment