VIONGOZI wa Chama cha ACT-Wazalendo pamoja na mwanahabari Haruna Mapunda, wamekwama kufikishwa mahakamani kutokana na jalada lao kupelekwa kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa na Wakili Bonifasia Mapunda anayewawakilisha watuhumiwa hao akiwemo Mbarala Maharagande, Katibu wa Kamati ya Uadilifu ACT, Mwikizu Mayama, Mwenyekiti wa ACT Jimbo la Ilala na Said Mohamed, Katibu wa Ngome ya Vijana Jimbo la Temeke.
Wakili Mapunda amesema, kutokana na jalada hilo kupelekwa kwa mwanasheria mkuu wa serikali, kuna uwezekano mkubwa watuhumiwa hao wakaendelea kusota rumande.
“Nimefika Polisi Chang’ombe asubuhi hii kuhakikisha kama mwandishi Mapunda na viongozi wetu Maharagande, Mwikizu na Mohamed leo wanapelekwa mahakamani.
“Taarifa niliyopewa ni kuwa jalada lao limepelekwa kwa mwanasheria wa serikali.Hivyobasi, Kuna uwezekano mkubwa leo bado wakaendelea kushikiliwa kituoni,” amesema Wakili Mapunda.
Aidha, Wakili Mapunda amesema anawasiliana na Jeshi la Polisi mkoa wa Kipolisi Temeke kwa ajili ya suala la dhamana la watuhumiwa hao.
“Ninasubiri kumuona mpelelezi mkuu kuhusiana na dhamana kabla ya kuchukua hatua nyingine za kisheria,” amesema Wakili Mapunda.
Watuhumiwa hao wanashikiliwa na Jeshi la Polisi tangu tarehe 24 Agosti 2019 katika Kituo cha Polisi Chang’ombe wakituhumiwa kufanya maandamano kinyume na sheria.
Watuhumiwa hao leo walitarajiwa kupandishwa kizimbani katika Mahakama ya Wilaya ya Temeke.
Leave a comment