SERIKALI imesema inatekeleza programu ya miaka mitano ya kukuza ujuzi inayolenga kuwezesha vijana 4,419,074 kupata ujuzi wa kuajiliwa au kujiajiri katika sekta mbalimbali, anaandika Dany Tibason.
Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI, Selemani Jafo akijibu swali la Mbunge wa wa Viti Maalum, Rodha Kunchela (Chadema) lililohoji serikali ina mikakati gani ya kusaidia vijana ili waweze kupata ajira na kujikwamua kiuchumi.
Kunchela aliihoji serikali bungeni wakati aliuliza swali la msingi kwa lengo ya kutaka kujua nini mikakati ya serikali kuwawezesha vijana katika kuwakwamua katika umasikini.
“Ipo changamto kubwa ya ukosefu wa ajira kwa vijana wa mkoa wa Katavi, ikichangiwa na miundombinu mibovu inayosababisha wawekezaji kushindwa kuwekeza.
“Je serikali ina mikakati gani ya kusaidia vijana hao wapate ajira na kuwa na mazingira wezeshi ya kujikwamua kiuchumi,” alihoji.
Jafo, amesema serikali ina mikakati ya kuhakikisha vijana wa mkoa wa Katavi na Tanzania kwa ujumla wanawezeshwa katika kupata mitaji na kuandaliwa mazingira rafiki.
Amesema serikali inazielekeza Mamlaka za serikali za Mitaa kuzingatia masuala ya ukuzaji wa ajira katika mipango ya maendeleo hususani kutambua na kubaini mahitaji ya nguvu kazi katika maeneo husika.
Amesema pia kuna kila sababu ya kutenga na kuendeleza maeneo ya uzalishaji biashara kwa vijana ili kuwezesha nguvu kazi kuwa na ujuzi wa kujiajiri, kuwezesha upatikanaji wa mitaji na vitendea kazi kwa makundi ya vijana, kukuza soko la bidhaa na huduma za wajasiliamali hasa vijana.
Amesema serikali inatekeleza programu ya miaka mitano ya kukuza ujuzi inayolenga kuwezesha vijana 4,419,074 kupata ujuzi wa kuajiliwa au kujiajiri katika sekta mbalimbali.
Amesema katika mwaka wa fedha 2016/7 vijana 1,469 wamepatiwa mafunzo ya ushonaji wa nguo kupitia viwanda vya mavazi.
Leave a comment