MAKUNDI mawili ya vijana wapatao 40 kutoka wilaya ya Kilosa mkoani hapa wamepatiwa msaada wa vifaa mbalimbali vyenye thamani ya Sh. 10 milioni ili kujiinua kiuchumi, anaandika Christina Haule.
Akikabidhi msaada huo Mkurugenzi mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Vijana na Wanawake Mafiga mkoani Morogoro (Mwayodeo), Venance Mlali amesema lengo la shirika hilo ni kuwasaidia vijana wenye umri wa kati ya miaka 18-30.
Amesema vijana hao watasaidiwa kwa kupatiwa elimu ya biashara kupitia mradi wa kuwapa elimu vijana kuhusiana na masuala ya ajira (OYE) na hatimaye kuwaingiza kwenye ujasiliamali na kuwaondoa tatizo la ajira kwa wilaya za Mvomero, Kilosa na Gairo mkoani Morogoro.
Mlali amesema kwamba vikundi vilivyapata vifaa hivyo ni vile vinavyojihusisha na utengenezaji wa majiko sanifu na masuala ya umeme wa jua vyote vikiwa vya wilaya ya Kilosa kutoka kata ya Magole na Ludewa ambavyo vyote vina vijana wapatao 20.
Amesema kuwa kwa ushirikiano na Shirika la Misaada la Uholanzi (SNV), wametoa maboksi ya tochi za aina mbalimbali na vifaa vya umeme wa sola ambao kikundi kimoja kitatumia kuchaji simu za jamii inayowazunguka na kuingiza fedha huku kikundi kingine kikipatiwa seti ya Tv ambayo wataitumia kuonesha picha mbalimbali kwa jamii na kukusanya fedha zitakazowasaidia.
Aidha, amesema makundi hayo yamepewa zawadi hizo kufuatia mashindano ya ujuzi yaliyofanyika mweza Januari mwaka huu huku makundi manne katika wilaya za Kilosa na Mvomero yakishiriki na makundi mawili kutoka katika wilaya ya Kilosa.
Leave a comment