TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) nchini Tanzania, imewafikisha Mahakama ya Kisutu jijini Dar es Salaam watuhumiwa watatu kati ya wanne waajiriwa wa Kampuni ya BEVCO LTD kwa tuhuma za rushwa na utakatishaji fedha zaidi ya Sh.1.6 bilioni. Anaripoti Mwandishi Wetu.
Taarifa iliyotolewa leo Alhamisi tarehe 19 Novemba 2020 na Afisa Habari wa Takukuru, Doreen Kapwani imesema, watuhumiwa hao wa kampuni hiyo inayojihusisha na uagizaji na uuzaji wa vinywaji vikali kutoka nje, wawili ni raia wa Tanzania na wengine wa Ufaransa.
Doreen amesema, uchunguzi wa awali uliofanywa na Takukuru umebaini, kampuni hiyo ambayo imesajiliwa Tanzania kwa ajili ya biashara hiyo tangu mwaka 2017, katika kutekeleza shughuli zake za biashara, wamekuwa wakichepusha Kodi ya Ongezeko laThamani (VAT) ambayo ilipaswa kulipwa serikalini.
Amesema, vitendo hivyo vya kihalifu, watuhumiwa wote wanne walikwepa kodi ya Sh.1.65 bilion na kuzitakatisha.
Amewataja watuhumiwa hao ni; Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo, Thiery Lefuevre na Meneja Rasilimali Watu, Melanie Phillippe ambao wote ni raia wa Ufaransa.
Mwingine ni, Ntemi Massanja, Mwanasheria wa BEVCO kutoka Kampuni ya Gabriel & Company Anttornys-AT Law huku Joseph Rwegasira Samson akiendelea kutafutwa.
“Atakayefanikisha kukamatwa kwa mtuhumiwa huyu, atapewa donge nono la Sh.10 milioni,” amesema Doreen
Ametaja makosa ambayo wanatuhumiwa nayo ni; kughushi, kuwasilisha nyaraka za uongo kwa mamlaka, kula njama ya kutenda kosa la uhujumu uchumi, kushindwa kulipa kodi ya ongezeko la thamani, kuisababishia serikali hasara na kutakatisha fedha.
Uchaguzi wa mwaka huu jinsi ulivoendeshwa itakuwa ndo mwisho watu kupiga kula la sivyo tume mpya iuundwe.