NAIBU Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Omary Kipanga amewasimamisha kazi maafisa wanne wa Chuo cha Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) Mkoa wa Lindi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Lindi … (endelea).
Kipanga amefikia uamuzi huo jana Jumamosi tarehe 9 Januari 2021, wakati alipokuwa akikagua mradi wa ujenzi wa Chuo cha VETA cha wilaya ya Mafia Mkoa wa Pwani ambacho ujenzi wake unasimamiwa na Chuo cha VETA Lindi.
Naibu waziri huyo, ameagiza, ofisi ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mafia na Lindi kuwachunguza iwapo hawakuwa na maslahi binafsi katika kusimamia ujenzi wa mradi huo.
Watumishi hao waliosimamishwa ni; Mkuu wa chuo, Cleophas Sikada; Afisa Ugavi na manunuzi, Daniel Solomon; Mhasibu,Richard Shekidele na Mkaguzi wa ndani ambaye jina lake halijafahamika.
Kipanga alisema, amechukua hatua hiyo baada ya kugundua ukiukwaji mkubwa wa taratibu katika kutunuku zabuni ikiwemo kumtunuku mwalimu wa chuo cha VETA Lindi, Rose Mlelwa na mafundi kufanya kazi bila ya mikataba.
“Kuanzia leo (jana) nawasimamisha kazi Mkuu wa VETA Lindi, Afisa manunuzi, Mhasibu na Mkaguzi wa ndani ili kupisha uchunguzi na nawaagiza Takukuru Mafia mshirikiane na Lindi kuwachunguza hawa ili tujue kama hawakuwa na maslahi binafsi kwenye mradi huu,” alisema Kipanga.
Aidha, aliwasimamisha mafundi wote waliopewa kazi ya ujenzi wa majengo zaidi ya moja na kuwataka kila mmoja ajenge jengo moja tu kama utaratibu unavyotaka, kutokana na mafundi hao kutokuwa na nguvukazi ya kutosha kukamilisha ujenzi kwa wakati uliopangwa.
Kipanga ambaye pia ni Mbunge wa Mafia (CCM) aliwataka wanaosimamia mradi kuhakikisha wanapatikana mafundi wengine haraka ili kukamilisha ujenzi huo ambao alidai haufahamiki utamalizika lini.
“Nataka mafundi wote waliopewa kazi ya kujenga zaidi ya jengo moja wabakie na ujenzi wa jengo moja tu, sababu hawana uwezo wa kutosha kukamilisha ujenzi kwa wakati na hivyo watasababisha ujenzi kuzidi kuchelewa,” amesisitiza mhe Kipanga.
Awali, akisoma taarifa ya ujenzi kwa niaba ya Mkuu wa chuo cha VETA Lindi, Richard Shekidele alisema, mpaka sasa kiasi cha Sh.1.1 bilioni kimeshapokelewa kwa ajili ya mradi huo na ujenzi umefikia asilimia 31.5.
Leave a comment