Tuesday , 16 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Upinzani Tanzania waivaa Tume ya Uchaguzi 
Habari za SiasaTangulizi

Upinzani Tanzania waivaa Tume ya Uchaguzi 

Spread the love

MUUNGANO wa vyama Nane vya upinzani nchini, umetuhumu Tume ya taifa ya uchaguzi (NEC), kuvunja katiba na sheria za nchi, kwa kuendelea kung’ang’ania wakurugenzi wa halmashauri, majiji na manispaa, kusimamia chaguzi zinazofanyika nchini. Anaripoti Faki Sosi … (endelea). 

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, leo Jumapili, 2 Juni 2019, mwenyekiti wa chama cha United Peoples Democratic Party (UPDP), Fahami Dovutwa, ameituhumu NEC kuendelea kuwatumia wakurugenzi hao kusimami uchaguzi, wakati tayari wamezuiwa na mahakama.

Amesema, “NEC imeendelea kudharau amri halali zinazotolewa na mamlaka za katiba. Pamoja na amri ya Mahakama Kuu ya kuwazuia wakurugenzi wa halmashauri, kusimamia uchaguzi, bado tume ya uchaguzi imeendelea kuwang’ang’ania kusimamia chaguzi zetu.

“Kitendo hiki, kinaonyeesha siyo tu, kwamba NEC, siyo chombo huru, bali pia hakiheshimi utawala wa sheria na mamlaka zilizopewa idhini kwa niaba ya wananchi.”

Amesema, kufuatia hali hiyo, chama chake cha UPDP, pamoja na vyama vingine vinane, vimeapa kutoshiriki chaguzi zozote zinazoitishwa na NEC na kusimamiwa na wakurugenzi wa halmashauri.

Vyama vingine ambavyo vimeapa kutoshiriki chaguzi hizo, ni Chama Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Alliance for Change and Transparency (ACT-Wazalendo),The National Convention for Construction and Reform (NCCR- Mageuzi), Chauma, National League for Democracy (NLD), Chama cha Kijamii (CCK) na Democrat Party (DP).

Hatua ya upinzani kususia chaguzi, inakuja mwezi mmoja tangu Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam, kuzuia wakurugenzi wa halmashauri, majini na manispaa, kusimia chaguzi za madiwani, wabunge na rais nchini Tanzania.

NEC imetangaza marudio ya chaguzi ndogo katika kata 32 nchini. Chaguzi katika kata hizo, umepangwa kufanyika tarehe 15 Julai mwaka huu.

Katika uamuzi wake, jopo la majaji watatu wa mahakama kuu wakiongozwa na Jaji, Dk. Atunganile Ngwala walisema, kifungu cha 7 (1), kinachompa mamlaka wakurugenzi wa halmashauri kusimamia uchaguzi, kinapingana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano.

Jaji Dk. Ngwala, ameeleza katika uamuzi huo kuwa kifungu cha 7 (1), kinapingana na Ibara ya 21 (1) na (2) na Ibara ya 26 (1), inayozungumzia ushiriki wa uchaguzi.

Amesema, vifungu hivyo vinakwenda kinyume na katiba kwa kuwa vinaruhusu wakurugenzi ambao baadhi yao, ni wanasiasa wa moja kwa moja, kusimamia chaguzi nchini.

Majaji wengine waliosikiliza shauri hilo, lililotolewa uamuzi tarehe 10 Mei 2019, ni Dk. Benhajj Masoud na Firmin Matogolo.

Aidha, Ibara ya 74 (14) ya Katiba ya Jamhuri, inaeleza kuwa “ni marufuku kwa watu wanaojishughulisha na uchaguzi, kujihusisha na vyama vya kisiasa.”

Katiba imewataja watu wanaojihusisha na uchaguzi, kuwa ni pamoja na wasimamizi wa uchaguzi katika ngazi ya wilaya na majiji.

Akisisitiza hoja yake, Dovutwa anasema, wakurugenzi wa halmashauri na manispaa ambapo uchaguzi huo mdogo wa madiwani unanyika, wamekuwa wakiandika barua kuarifu maandalizi ya chaguzi hizo; na ndio wamekuwa wakizisaini kama wasimamizi wakuu.

“Hawa wakurugenzi waliopigwa marufuku na mahakama, ndio wanaoandika barua kwa vyama vya siasa, kuviarifu juu ya mchakato wa kuchukua na kurejesha fomu. Barua zote zimesainiwa na wao kama wasiamizi wakuu wa uchaguzi. Hii kwa maoni yetu, ni kinyume na katiba na ni kudharau mahakama,” ameeleza.

Amesema, “hivyo basi, sisi hatutashiriki uchaguzi huo. Kwani kufanya hivyo, ni sawa na kubariki dharau kwa mahakama inayooneshwa na NEC.”

Dovutwa anasema, ili kukabilina na “dharau ya NEC kwa mahakama,” wameamua kuwasilisha shauri mahakamanai kukazia hukumu iliyotolewa tarehe 10 Mei 2019.

Amesema, “tumekubaliana pamoja na wanaharakati walioendesha kesi hiyo, wakiwemo Bob Chaha Wangwe, kuwapa ushirikiano wa kina, ili kuweza kuwasilisha shauri hilo mahakama kuu; kukazia hukumu ya mahakama na kuitaka mahakama kuichukulia hatua NEC kwa kitendo chake cha kudharau muhimili huo.”

Amesema, “tunatambua kuwa uchaguzi huo wa madiwani unasimamiwa na sheria ya uchaguzi wa serikali za mitaa chini ya sheria ya uchaguzi wa mwaka 1985. Hivyo, tunaitaka NEC kutumia mamlaka yake iliyopewa na Katiba, Ibara 74 (15) (e), kulifuta zoezi linaloendelea ili kuteua wasimamizi huru wa uchaguzi huu wa marudio.”

Katika siku za hivi karibuni, kumeibuka kilio cha kuwapo tume huru ya uchaguzi, kufuatia baadhi ya wakurugenzi wa halamshauri, kuonekana dhahiri shahiri, kukipendelea Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

CAG abaini madudu katika vyama 10 vya upinzani

Spread the loveUKAGUZI wa Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali...

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

‘Mwanapekee’ wa Rais Samia: Atabadili nini Arusha?

Spread the loveMAPEMA wiki hii, baadhi ya viongozi walioapishwa na Rais Samia...

Habari za Siasa

Hivi kweli Ole Sendeka alishambuliwa kwa risasi?

Spread the loveMIMI siamini kwamba yupo mtu mwenye nia ya kuua ambaye...

Habari za SiasaTangulizi

Makonda kung’oka tena

Spread the loveUWEZEKANO wa Paul Makonda, kuendelea na wadhifa wake wa mkuu...

error: Content is protected !!