DAKTARI Faustine Ndugulile, Naibu Waziri wa Afya amesema, ugonjwa wa corona (COVID-19) unatesa zaidi wenye kinga dhaifu. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam … (endelea).
Akizungumza katika mahojiano yake na Kituo cha Televisheni cha ITV leo tarehe 17 Machi 2020, amesema ugonjwa huo hauna athari kubwa kwa watu wenye kinga imara za mwili.
Dk. Ndugulile ameeleza, ugonjwa huo ukimuingia mtu mwenye kinga imara, huisha wenyewe ndani ya siku saba hadi 10.
“Ugonjwa huu wa corona bahati mbaya hauna tiba, ni ugonjwa ambao unaisha wenyewe baada ya siku saba mpaka 10, kama mtu kinga zake za mwili ziko vizuri ni ugonjwa ambao ndani ya siku saba mpaka 10 unaisha wenyewe,”amesema Dk. Ndugulile.
Aidha amesema, vifo vinavyotokana na virusi hivyo ni chinu ya asilimia tatu ya watu walioambukizwa ugonjwa huo.
“Vifo vinavyotokana na ugonjwa huu wa corona ni chini ya asilimia tatu ya watu wote ambao wamepata ugonjwa huo,” amesema Dk. Ndugulile.
Hata hivyo, amesema wazee na watu wenye magonjwa ya ziada, wako katika hatari kubwa ya maambukizi ugonjwa huo.
“Takwimu zinaonesha, kwamba kwa wale ambao wamepata ugonjwa huu wa corona na wale waliofariki, ni wazee ama watu waliokuwa na magonjwa ya ziada ambayo yaliwafanya miili yao kuwa dhaifu kidogo, hao mara nyingi huwa wanafariki,” ameeleza Dk. Ndugulile.
Na kwamba, serikali imejipanga vyema katika kukabiliana na janga hilo, na kitoa wito kwa Watanzania kupuuza taarifa za mitandaoni juu ya ugonjwa huo, badala yake wafuatilie taarifa zinazotolewa na mamlaka husika.
“Kila mtu siku hizi amekuwa ni msemaji, mwingine anasema kula vitunguu swaumu, sijui unywe juisi gani, vyote hivyo ni upotoshaji mkubwa sana kwa umma, tutaanza kuchukua hatua kwa wanaosambaza,”amesema Dk. Ndugulile.
Leave a comment