WAFANYABIASHARA wametakiwa kufuata utaratibu na kutumia mizani iliyohakikiwa na Wakala wa Vipimo Tanzania (WMA) ili waweze kuuza bidhaa kihalali na kuepuka kuwapunja wateja jambo ambalo ni kinyume cha sheria. Anaripoti Christina Haule … (endelea).
Kaimu Meneja wa WMA mkoa wa Morogoro, Dismas Maturine amesema, kufuatia kuibuka kwa watengenezaji wa mizani feki kwa sasa wafanyabiashara wanaouza bidhaa na mizani yenyewe hawana budi kuhakiki mizani kabla ya kuinunua.
Amesema kuwa WMA ina utaratibu wa kukagua mizani yote inayoingizwa nchini ambapo imekuwa ikibaini baadhi ya mizani ambayo ni feki kufuatia kutokuwa na lebo (stika) halisi ya WMA na kutokuwa na muhuri unaopaswa kugongwa na WMA kila mwaka kisheria.
Ameongeza kuwa wanautaratibu wa kukagua kwa awamu mizani iliyopo kwenye maduka ili kumfanya mteja kupata bidhaa kinacholingana na thamani ya fedha aliyotoa kisheria.
“Tumeshawahi kukamata mizani 100 katika kiwanda bubu kilichokuwa kikitengeneza mizani hiyo jijini Dar es Salaam na kilichukuliwa hatua kisheria na mwaka huu 2018 tumekamata mizani miwili ambapo kesi ipo polisi na wanatarajia kuifikishwa mahakamani,” amesema.
Maturine amesema ni kosa kisheria kwa muuzaji wa bidhaa au mizani yenyewe kuuza bidhaa feki ambapo mtu akikamatwa ana mzani feki anatozwa faini ya kuanzia Sh. 100,000 hadi Sh. 20 milioni.
Aidha amesema kuwa mtu huyo huyo akikamatwa kwa mara ya pili na kosa hilo hilo atafikishwa mahakamani na kutozwa kiasi cha Sh. 300,000 hadi Sh. 50 milioni faini ambayo imepanda tangu mwaka 2016 ambapo awali ilikuwa ni sh 10,000.
Amesema kuwa licha ya kubadilisha ubora wa mizani kila baada ya miaka kadhaa lakini wauzaji wa mizani feki nao wamekuwa na tabia ya kutengeneza mipya kulingana na iliyopo.
“Watengenezaji wa mizani feki wapo kama watengenezaji wa fedha bandia kwa sababu wanatengeneza kila toleo linalotolewa na watengezaji wa mizani halali,” amesema Maturine.
Akizungumzia tatizo la mizani feki mteja wa bidhaa madukani Victor Makinda amesema kuwa licha ya kupima chini ya kiwango ambacho hakiendani na thamani ya fedha inayotolewa ni dhambi mbele za mungu kufanya hivyo lakini pia wafanyabiashara wanatakiwa kuona umuhimu wa kupima kihalali ili kumfanya mnunuzi kwenda sambamba na hali ya uchumi uliopo kwa sasa.
Hivyo amesema Serikali izimarishe Taasisi zinazofanya ukaguzi wa mizani ili ziweze kutembelea maeneo husika na kubaini mizani feki iliyopo ili kuweza kukomesha tatizo hilo.
Leave a comment