ERICK Kabendera, Mwanahabari aliyeko Mahabusu katika Gereza la Segerea jijini Dar es salaam, ametoa ujumbe mzito kufuatia kuzuiwa kutoa heshima za mwisho, kwa Marehemu Mama yake, Verdiana Mujwahuzi. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Mwanahabari huyo anayetuhumiwa kwa mashtaka ya utakatishaji fedha na uhujumu uchumi, amesema uchungu wa kuondokewa na mama ni mkubwa, hasa kwa mtu aliyekosa fursa ya kutoa heshima za mwisho, kama ilivyotokea kwake.
Ujumbe huo wa Kabendera umetolewa leo tarehe 3 Januari 2020, na Zitto Kabwe, Kiongozi Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo, kwa niaba ya Jebra Kambole, Wakili wa mtuhumiwa huyo, katika ibada ya kuuaga mwili wa Mama Mujwahuzi, iliyofanyika Kanisa Katoliki Chang’ombe, Dar es Salaam.
Kabendera ameeleza kuwa, duniani kuna mama mmoja, anayefariki mara moja na msiba wake huwa ni mmoja tu, hivyo kuzuiwa kumpa heshima ya mwisho mama yake, kumemuumiza sana.
“Kuna mama moja tu, anafariki mara moja tu, msiba mara moja tu. Uchungu wa kuondokewa na mama ni mkubwa sana, hasa anapokuwa anaondoka na kushindwa kumuaga kama ilivyotokea kwangu,” ujumbe wa Kabendera kama ulivyofikishwa kwa umma na Zitto.
Kabendera amewashukuru watu walioguswa na msiba wa mama yake, bila kujali tofauti zao za kiitikadi.
“Hata hivyo nimeguswa na watu walivyo upokea msiba huu bila kujali itikadi zao za kisiasa na kidini na kumzika mama yangu,” unaeleza ujumbe wa Kabendera, uliotolewa na Zitto.
Leave a comment