UJENZI wa darala jipya la Wami unaogharamiwa na serikali ya Tanzania kwa asilimia 100, umefika asilimia 37.5 ili kukamilika. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Injinia Izack Kamwele, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ametoa kauli hiyo leo tarehe 13 Mei 2020, wakati akijibu swali la Zainab Mndolwa Amri, Mbunge Viti (CUF)
Zainab aliuliza, ni lini serikali itatafuta wawekezaji wa kujenga daraja la Wami, Mkoa wa Pwani ili liwe la kisasa na liweze kutoza tozo kwa watumiaji wa vyombo vya moto kama ilivyo kwa daraja la Kigamboni, Dar es salaam?
Akijibu swali hilo, Inj. Kamwele amesema, upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa daraja jipya la Wami ulikamilika Machi 2016.
“Daraja la Wami limesanifiwa kuwa na urefu wa mita 513.5 na upana wa mita 11.85, na litajenga umbali wa mita 670 pembeni mwa daraja linalotumika sasa,” amesema Kmwele na kuongeza:
“Upana wa daraja hilo umezingatia sehemu ya barabara, watembea kwa miguu pamoja na vizuizi kwa ajili ya usalama. Mkataba wa ujenzi wa daraja jipya la Wami ulisainiwa tarehe 28/6/2018, kati ya Serikali na Mkandarasa Power Construction Corporation wa China kwa muda wa miezi 24.”
Amesema, ujenzi huo utajumuisha ujenzi wa barabara unganishi kwa pande zote mbili zenye jumla ya urefu wa kilometa 3.82, ili kuweza kuunganisha daraja jipya na barabara kuu ya Chalinze – Segera.
Leave a comment