Friday , 29 March 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Uhujumu uchumi NIDA: TAKUKURU wamtaka kumhoji upya mtuhumiwa
Habari za SiasaTangulizi

Uhujumu uchumi NIDA: TAKUKURU wamtaka kumhoji upya mtuhumiwa

Spread the love

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, imeombwa kufanya mahojiano upya na Xavery Kayombo, anayeshitakiwa kwa kosa la kuhujumu uchumi wa taifa. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).

Kayombo ni mshitakiwa Na. 5 kwenye kesi hiyo inayomkabili pia Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), Dickson Maimu. 

Mshtakiwa huyo anatakiwa kuhojiwa upu kwenye tuhuma ambazo Wakili wa serikali kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Leornad Swai amesema, hajawahi kuhojiwa nazo.

Mbele ya Hakimu Mkazi wa mahakama hiyo, Salum Ally, ameiomba mahakama kuwa TAKUKURU inamuhitaji Kayombo ili waweze kumhoji kwenye tuhuma mpya zinazomkabili.

Washtakiwa wengine katika kesi hiyo, ni Meneja Biashara wa (NIDA), Aveln Momburi; Mkurugenzi wa kampuni ya Aste Insurance Brokers,  Astery Ndege; Ofisa Usafirishaji, George Ntalima na Sabina Raymond.

Washtakiwa hao  wanakabiliwa na mashtaka 22 ya kughushi, mashtaka 43 ya kutumia nyaraka kwa lengo la kumdanganya mwajiri, mashtaka mawili ya kula njama, mashtaka 25 ya kutakatisha fedha na mashtaka matano ya kuisababishia hasara NIDA.

Aidha, washtakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka mawili ya kufoji ili wapate fedha kwa njia ya udanganyifu na shtaka moja la matumizi mabaya ya madaraka ambalo linamkabili  Maimu na Sabina.

Hoja ya kutaka Kayombo ahojiwe, ilipingwa na wakili wa utetezi Benjamin Mwakagamba, kwa maelezo kuwa tayari rekodi za mahakama zinaonyesha upelelezi wa shauri hilo umeshakamilika, ikiwa ni pamoja na kuwahoji washitakiwa.

“Tumeambiwa hapa mahakamani kuwa upelelezi umekamilika na upande wa mashitaka uko tayari kuleta mashahidi wake kwenye shauri hili. Wala mahakama haijaelezwa sababu za msingi za kuleta maombi haya mapya,” alieleza Mwakagamba.

Alisema, “ni rai yetu, ombi hili halina nia nyingine, bali ni kutaka kuchelewesha usikilizwaji wa shauli hili. Hivyo basi, tunaomba mahakama ilikatae. ”

Baada ya mabishano hayo ya kisheria, Hakimu Ally alisema amezisikia hoja za pande zote mbili na anakubali kuwa kwa hatua ilipofikia kesi hiyo, washtakiwa wameishahojiwa na kutoa maelezo yao.

Amesema, kwa kuwa upande wa mashtaka umesema bado wapo katika hatua za mwisho za kuwasilisha taarifa Mahakama Kuu, haoni sababu ya kuzuia mshtakiwa wa tano kuhojiwa na Takukuru.

Hata hivyo, aliruhusu kufanyika kwa mahojiano hayo leo tarehe 12 Februari 2019, kabla muda wa washtakiwa kurudi gerezani haujamalizika.

Alisema, “tunaomba mahojiano haya yafanyike leo tu, mpaka muda wa kuwarudisha mahabusu mshtakiwa huyu awe amekwishamaliza kuhojiwa ili kuondoa wasiwasi kuwa kuna nia ya ucheleweshaji wa kesi.”

Awali wakili Swai aliieleza mahakama kuwa kesi hiyo ilikuja kwa ajili ya kutolewa maelezo ya mashahidi na kwamba wapo katika hatua za mwisho za kuwasilisha taarifa kwa ajili ya kuwasomea washtakiwa yao.

Baada ya kesi hiyo kiahirishwa, nje ya mahakama ndugu, jamaa na marafiki wa washtakiwa walisikika wakiangua vilio.

Miongoni mwa malalamiko yao, ni kitendo cha kesi hiyo kuendeshwa katika mahakama ya ndani(Chamber), badala ya mahakama ya wazi.

Walisema, hatua hiyo imewafanya kutopata nafasi ya kuwaona ndugu zao ambao kutokana na mashtaka yao, hawawezi kupata dhamana katika Mahakama ya Kisutu.

“Tumetoka mbali sana, wapo waliotoka Mbeya pia wengine Kibamba,  Mbezi yote hiyo ni kwa ajili ya kutaka kusikiliza kesi ya ndugu zetu ila tunashangaa kuona imeitwa chamber.

“Nini wanatuficha tusijue kinachoendelea? Jambo hili limetusikitisha na kutuumiza, ” alisikika mmoja wa ndugu hao.

Kufuatia tukio hilo, polisi waliwatawanya ndugu, jamaa na marafiki waliokuwapo mahakamani hapo.

 

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

Nani anasema kuna hasara ATCL?

Spread the loveRIPOTI za makusanyo na matumizi ya fedha katika Kampuni ya...

Habari za SiasaTangulizi

CAG: Wastaafu, wenza wao chanzo NHIF kufilisika

Spread the loveRIPOTI ya ukaguzi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu...

Habari za SiasaTangulizi

Vikundi hewa 851 vyalamba bilioni 2.6 mikopo ya halmashauri

Spread the loveVIKUNDI hewa vya wajasirimali wadogo 851 kutoka katika halmashauri 19...

Habari za SiasaTangulizi

Mashirika matano yapata hasara mabilioni ya fedha

Spread the loveMASHIRIKA matano ya Serikali yanayojiendesha kibiashara, yamepata hasara ya mabilioni...

error: Content is protected !!