MWENYEKITI wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe ameshindwa kufika katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kutokana na kuwa nje ya nchi kwa ajili ya matibabu ya ugonjwa wa moyo na shinikizo la damu. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Mdhamini wa Mbowe, Grayson Celestine ameieleza mahakama akidai kuwa, aliwasiliana na mke wa Mbowe jana ambaye alimueleza kwamba, Mbowe amesafirishwa kwa dharula nje ya nchi na familia yake, kwa ajili ya kupatiwa matibabu.
Kuali hiyo ilitolewa baada ya Mbowe ambaye ni mshtakiwa wa kwanza katika kesi ya jinai Na. 112/2018, kushindwa kupanda kizimbani huku washtakiwa wengine wanane wakipanda kizimbani katika mahakama hiyo.
Kutokana na Mbowe kutohudhuria mahakamani, Wakili Mkuu wa Serikali, Faraja Nchimbi aliiomba mahakama kutoa amri, Mbowe akamatwe ili aeleze kwa nini dhamana aliyopewa isifutwe kutokana na kushindwa kufika mahakamani.
#KesiUpdatesKisutu Mhe @freemanmbowetz ni mgonjwa mahututi amesafirishwa kwa dharura kupelekwa kwenye matibabu Afrika Kusini, wakili wake aitaarifu mahakama.
— CHADEMA Tanzania (@ChademaTz) November 1, 2018
Kufuatia hoja hizo, Hakimu Wilbard Mashauri alihoji kama Mbowe ana uthibitisho kwamba alisafiri nje ya nchi kwa ajili ya matibabu, na kujibiwa na Celestine akidai kuwa mtuhumiwa huyo akirejea nchini atawasilisha nyaraka za safari na matibabu.
Hakimu Mashauri amesema endapo Mbowe hatopeleka uthibitisho mahakani hapo, atatoa amri ya kumkamata ili ajieleze kwa nini asifutiwe dhamana kwa kukiuka masharti ya dhamana aliyopewa na mahakama.
Leave a comment