JOTO la Uchaguzi wa urais, wabunge na wawakilishi utakaofanyika Oktoba 2020, visiwani Zanzibar, limepamba moto huku kukiwa na tuhuma za vyama vya upinzani, kufanyiwa figisu na Tume ya Uchaguzi (ZEC). Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea).
Ikiwa imebaki takribani miezi minne kwa uchaguzi huo kifanyika, Chama cha ACT-Wazalendo, kimetoa tuhuma dhidi ya ZEC, ya kwamba tume hiyo inaandaa mikakati ya kubeba Chama cha Mapinduzi (CCM), ili kipate ushindi katika uchaguzi huo.
Salim Bimani, Katibu Habari, Uenezi, Mahusiano na Umma wa ACT-Wazalendo, amedai, ZEC ina mkakati wa kupunguza idadi ya majimbo katika maeneo ambayo vyama vya upinzani vina nguvu.
Bimani alitoa tuhuma hizo jana Jumatatu tarehe 1 Juni 2020, wakati akizungumza na Mwanahalisi Online kwa simu.
Tuhuma hizo zimeibuka baada ya ZEC hivi karibuni kutoa tangazo la kuwataka wadau wa uchaguzi, ikiwemo vyama vya siasa, kutoa mapendekezo yao juu ya upitiaji majimbo.
“Hatukubaliani kwa sababu moja ya msingi, ukataji wa majimbo, moja hufanywa na sense, hakuna sensa iliyofanyika. Lakini kuna vigezo mbalimbali vya ukataji majimbo vinafanywa kwa kushirikishwa na wananchi wenyewe kwa kuzingatia mambo muhimu,” alisema Bimani
“Tumeona idadi kubwa ZEC inafanya kwa mtizamo wa kisiasa. Zanzibar kulikiwa na majimbo 50, 21 pemba 29, baada ya upinzani kuchukua viti vyote Pemba ZEC ilipunguza majimbo kutoka 21 hadi kufikia 18. Walifanya hivyo mwaka 2000 walipunguza.”
Bimani alidai, kitendo cha majimbo kupunguzwa, kinawanyima uwakilishi wananchi wa maeneo husika.
“Wanataka kupunguza majimbo Pemba kuongeza Unguja. Inawanyima uwakilishi wananchi wa Pemba ndani ya baraza la wawakilishi au bungeni. Tunataka yabaki majimboni 21 Pemba kama yaliyokuwa,” amesema Bimani.
Kufuatia madai hayo, Mwanahalisi Online ilimtafuta kwa simu, Thabiti Idarous Faina, Mkurugenzi wa ZEC, kwa ajili ya ufafanuzi wake, ambaye alisema hana taarifa rasmi juu ya malalamiko hayo.
Faina alisema, hana taarifa juu ya tuhuma hizo kwa kuwa yuko nje ya ofisi yake akitekeleza majukumu mengine ya ZEC, na kwamba akirejea, atatoa ufafanuzi wake, kama ACT-Wazalendo itakuwa imewasilisha malalamiko yao kwa njia ya maandishi.
“Unajua kwa bahati mbaya hilo tangazo ulilotamka sijaliona naogopa kuwa mnafiki katika maelezo yangu. Lakini hilo tangazo (upitiaji majimbo) lilikuwepo na kwa bahati nzuri au mbaya hao ACT nao pia wameleta maoni yao,” alisema Faina
“Sasa sitaki kusema sababu sijaona unachokisema, naomba nipe muda tarehe 4 Juni 2020 nitakuweoo Zanzibar kwa ajili ya kufuatilia zaidi kile ambacho unakizungumza.”
Faina alisema, pindi atakapopata malalamiko hayo kwa njia ya maandishi, atayatolea ufafanuzi.
“Nimetoka kwenye uandikishaji Pemba nikirudi Unguja nitakuwa na maelezo mazuri kama watakuwa wametuletea, tutalisema vizuri hilo suala, lakini kama unavyosema tuhuma zitakazoletwa kwetu kwa njia ya maandishi tutazijibu kama walivyotuletea kwetu,” alisema Faina.
Baada ya maelezo hayo ya ZEC, MwanaHALISI ONLINE lilimtafuta tena, Bimani ambaye alisema, ACT-Wazalendo imepeleka malalamiko yao katika ofisi za ZEC, kwa njia ya maandishi zaidi ya mara moja.
Leave a comment