VYAMA vya siasa nchini Tanzania, vimetakiwa kuweka mazingira sawa ya ushiriki wa wanawake, vijana na wenye umelavu katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Uchaguzi huo utahusisha madiwani, wabunge na wawakilishi upande wa Zanzibar pamoja na urais wa Tanzania na wa visiwa.
Tayari vyama mbalimbali vimekwisha kuanza michakato ya ndani ya kuwapata wagombea wa nafasi hizo huku Shirika lisilo la Kiserikali la Tanzania Youth Coalition (TYC) likifanya utafitri kuangazia ushiriki wa wanawake, vijana na wenye umelavu katika chaguzi zinavyokuwa.
Mshauri Mwelekezi wa TYC, Zatwa Nyingi alisema, katika utafiti huo, wamebaini ushiriki wa makundi hayo katika uchaguzi wa serikali za mitaa uliofanyika tarehe 24 Novemba 2019 ulikuwa hafifu.
Alisema, wamebaini ushiriki wao ulikuwa hafifu kidogo na wanaomba wawezeshwe ili uchaguzi ujao washiriki kikamilifu.
“Na kuwezeshwa kwao ni kupewa taarifa mapema, kupewa vitendea kazi, waelimishwe na wapewe fursa ya kujadili kuhusu sharia na michakato ya uchaguzi,” alisema Nyingi
Katibu wa Ushiriki Tanzania, Raymond Kanegene alisema, taratibu na miongozo ya vyama vingi vya siasa haviko shirikishi kwa makundi hayo hivyo, ni wakati wa kuboresha ili kutoa fursa sawa.
Alisema, hilo wamelibaini kupitia utafiti walioufanya na kukuta changamoto mbalimbali zinazowakuta wanawake, vijana na wenye ulemavu unaochangia kutojitokeza kushiriki.
“Tunatoa wito kwa vyama vya siasa, kuboresha katiba na miongozo yake bado kwa namna fulani haiko shirikishi kwa makundi hayo hivyo waboreshe ili kuweza kuzingatia makundi hayo kwenye uchaguzi,” alisema Kanegene
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa TYC, Lenin Kazoba alisema utafiti huo unalenga kuangalia jinsi wanawake, vijana na wenye ulemavu wanashiriki kikamilifu na maeneo gani yanayopaswa kuangaliwa.
Alisema utafiti huo, watautimia kuhamisha vyama vya siasa na wadau wengine kuhakikisha makundi hayo muhimum kwa jamii yanapata fursa kubwa na pana kwenye uchaguzi mkuu ujao.
Leave a comment