RAIS wa Jamhuri, Dk. John Magufuli amesema, ana imani kubwa ya uchaguzi mkuu ujao wa rais, wabunge na madiwani, kuwa huru na haki. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodom …(endelea).
Amesema, “…yule atakayechokoza kwa kufanya vurugu, basi atakuwa amejichokoza yeye. Mimi binafsi, nina imani kubwa, kwamba uchaguzi mkuu, utakuwa huru na mambo yote yatakwenda vizuri.”
Rais Magufuli ametoa kauli hiyo, leo Jumatano, tarehe 22 Julai 2020, wakati akizindua ofisi za Tume ya Uchaguzi ya Taifa (NEC), zilizopo eneo la Njedengwa, mkoani Dodoma.
Alikuwa akizungumzia umuhimu wa kuwapo utulivu kwenye uchaguzi huo. Amesema, vurugu hazijengi, badala yake zinabomoa. Akataka vyombo vya usalama kusimamia usalama wa raia wa Jamhuri ya Muungano.
Amesema, “navihimiza vyama vya siasa kushiriki kwenye uchaguzi huu na kuepuka kujiingiza kwenye vurugu,” ameeleza rais Magufuli na kuongeza, “vurugu hazijengi, vurugu zinaboma.”
Rais Magufuli amevitaka vyama vya siasa kufanya kampeni za kistaarabu huku akiwataka wananchi kujiandaa na uchaguzi huo.
Rais amesema, “…nimeona kuna vyama vingi sana; katika vyama hakuna vidogo sisi sote tuko sawa. Niviombe vyama hivi, viendeshe kampeni kistaarabu na mimi naahidi uwanja wa kisiasa utakuwa huru.”
Amevihakikishia vyama vya upinzani kuvipa ushirikiano wakati wote wa uchaguzi huo.
“Viongozi wa siasa, mimi ni mwenzenu. Tunajenga nyumba moja Tanzania; nataka niwathibitishie, nitatoa ushirikiano mzuri sana kwa vyama vyote, ili twende na maadili yetu kama tulivyofundishwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere,” amesisitiza.
Akizungumza kwa sauti ya upole, Rais Magufuli ameahidi uwanja wa kisiasa utakuwa huru kwa vyama vyote vitakavyoshiriki uchaguzi huo.
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na NEC, jana Jumanne, mchakato wa uchaguzi huo, utaanza rasmi kwa zoezi la uteuzi wa wagombea, litakalofanyika tarehe 25 Agosti 2020.
NEC imesema, kampeni za uchaguzi huo, zimepangwa kuanza 26 Agosti hadi 27 Oktoba mwaka huu, na kwamba uchaguzi mkuu utafanyika siku moja baadaye 28 Oktoba 2020.
Leave a comment