ALBERT Chalamila, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya (RC) amewachongea wateule wa Rais John Pombe Magufuli waliokimbilia kugombea nafasi mbalimbali za uongozi katika kinyang’anyiro cha Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Chalamila amesema hayo leo Alhamisi tarehe 16 Julai 2020 Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma katika halfa ya Rais John Pombe Magufuli kuwaapisha viongozi mbalimbali aliowateua wakiwemo wakuu wa mikoa, wilaya na katibu tawala.
Amesema, kitendo cha wateule wa Rais Magufuli kwenda kugombea kinaashiria hawana nidhamu mbele ya mamlaka zilizowateua.
Mara mbili Rais Magufuli aliwaonya wateule wake, kutoachia madaraka yao kwa ajili ya kujitosa katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020 na kuwataka waridhike na nafasi zao.
Katika nyakati tofauti Rais Magufuli aliwataka wateule wake kutoomba likizo kwa ajili ya kwenda kugombea katika uchaguzi huo.
Hata hivyo, alisema hatowalazimisha kusikiliza ushauri wake, lakini kufanikiwa kwao katika harakati zao hizo, kunategemea na yeye ataamkaje.
Akizungumzia ushauri huo wa Rais Magufuli, Chalamila amesema alimua kutii ushauri huo kwa kubadili msimamo wake wa kutaka kugombea.
“Baada ya Rais Magufuli kutoa kauli hiyo, nilijiuliza nikiondoka sijui kama nitakuwa nimetii na kuwa na nidhamu mbele ya mamlaka na sasa wananita Mzee wa U-tune,” amesema Chalamila.
Chalamila amesema, hata alivyozungumza na wanahabari na kueleza msimamo wake wa kutogombea katika uchaguzi huo, alitarajia wakuu wa mikoa na wateule wengine, wangefuata nyayo zake, kwa kuacha kugombea.
“Nilikaa nikatafakari sana, magazeti wakaniambia nimebaidili gia angani, nilimwambia Waziri Selemani Jaffo, nilieza maneno yale nikaamini pia wenzangu wachache watasikiliza, waliona nachekesha lakini leo wanashuhudia haikuwa kichekesho ilikuwa filamu halisi,” amesema Chalamila huku waliohudhuria wakifurahia
Chalamila amesema, wateule wa Rais Magufuli kwa sasa wanamsumbua kutokana na kuwa na mihemko ya kugombea kwenye uchaguzi huo na kumtaka kiongozi huyo kuendelea kuwavumilia wateule wake hao.
“Nilivyosema ilionekana ni vichekesho lakini tunakusumbua sana uendelee, kutuwia radhi sana. Usichoke kutulea vijana tunamiemko sana,” amesema Chalamila.
Naye Mkuu wa Majeshi la Ulinzi na Usalama (CDF), Venance Mabeyo amempongeza RC Chalamila kwa maneno mazuri kwa viongozi wanachukua uamuzi wa kwenda kugombea.
“Ni dhamana kubwa mnayokabidhiwa leo ambayo wengine tunayo na lengo ni kwenda kuwatumikia wananchi na kubwa kujitafakari na kujitambua ili tunapotumikia nafasi zetu tujue ni kwa ajili ya maendeleo ya Taifa na wananchi,” amesema Mabeyo
Amesema mkuu huyo wa mkoa wa Mbeya alijitafakari kabla ya kwenda kugombea na kuamua kuacha kutokana na ushauri wa Rais Magufuli.
Soma zaidi hapa
Rais Magufuli awaapisha warithi wa Makonda, Mnyeti
Mabeyo amesema, kwa mujibu wa taratibu za kazi, mtumishi wa umma anayetaka kwenda kugombea anapaswa kuacha kazi ili aende kugombea kwanza.
Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Seleman Jafo amewataka wateule hao kwenda kusimamia matumizi ya fedha na ukusanyaji wa mapato.
Waziri Jafo amewataka kwenda kufanya kazi kwa nguvu ili kumsaidia Rais Magufuli.
…toshekeni
Akizungumza katika halfa hiyo, Makamu wa Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amesema, “utawala wetu ni utawala wa utumishi wa watu siyo wa kuhaha na madaraka. Wale wakuu wa mikoa na wilaya nendeni kawatumikie watu siyo kuwaongoza.”
Amesema, mnakwenda kuwatumikia watu na mnapokwenda wengine mmetoka hapo hapo na wapya someni na mrekebishe. Kurekebisha ndiyo mafanikio.
“Nadhani mtajifunza kutokana na somo la RC Chalamila, kutosheka. Unatosheka na unachokipata,” amesema Samia
Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online na MwanaHALISI TV
Leave a comment