ANGELLAH Akilimali, Mkuu wa Idara ya siasa na habari wa vyombo vya habari vya Chama Cha Mapinduzi (CCM) amejitosa kuwania ubunge Ukonga. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam (endelea)
Angellah ambaye pia mwandishi wa habari mkongwe amechukua fomu Ofisi za CCM Wilaya ya Ilala leo Jumatano tarehe 15 Julai 2020 akiomba chama hicho kumpitisha kuwania ubunge jimbo la Ukonga jijini Dar es Salaam.
Mara baada ya kukabidhiwa fomu na Iddi Mkowa, Katibu wa CCM wilayani humo, Angella amesema, amejitosa kuomba ridhaa ya chama hicho ili kuwatumikia wana Ukonga.
“Kama mwanachama, nimetumia haki yangu kikatiba kuchukua fomu na nitarejesha na mwisho chama kitaendelea na mchakato utakapokamilika atapatikana mmoja,” amesema Angellah
Angellah amewahi kuwa kaimu mkurugenzi wa redio ya chama hicho redio Uhuru na Mjumbe wa Halmashauri Kuu CCM (NEC).
Kwa upande wake, Katibu wa CCM Wilaya ya Iddi Mkowa amesema Wilaya hiyo ina majimbo matatu ambapo hadi kufikia leo Jumatano saa 6 mchana, Ukonga wamejitokeza 85, Ilala 12 na Segerea 51.
Mkowa amewaomba wanachama wenye sifa za kuwania uongozi, waendelee kujitokeza.
Leave a comment