WANACHAMA 247 wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Iringa wamejitosa kuwania kupitishwa na chama hicho kuwania ubunge katika majimbo saba mkoani humo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Iringa…(endelea).
Idadi hiyo ni ya siku mbili tangu shughuli ya uchukuaji na urejeshaji fomu ulipoanza Jumatatu iliyopita tarehe 14 Julai 2020 hadi jana.
Akizungumza leo Alhamisi tarehe 16 Julai 2020, Katibu wa CCM Mkoa wa Iringa, Brown Mwangomale amesema, mwitikio umekuwa mkubwa kutokana na kukua kwa demokrasia ndani ya chama hicho tawala.
Akitaja idadi ya waliojitokeza ndani ya siku hadi jana, Mwangomale amesema ni 247.
Amesema, Iringa Mjini wako 44, Isimani saba, Kalenga 48, Kilolo 34, Mufindi Kaskazini 28, Mufindi Kusini watano, na Mafinga Mjini 15.
Aidha Mwangomale ameonesha kusikitishwa kutokana na mwamko mdogo wa wanawake pamoja na kundi la watu wenye ulemavu kutojitokeza kuwania kugombea.
Naye miongoni mwa waliojitokeza kuchukua fomu kuomba kupitishwa kugombea Mufundi Kusini, Josephat Mwagala amesema wingi wa wagombea unatokana na uhuru na uwazi.
Mwagala amesema katika chaguzi zilizopita mwitikio ulikuwepo lakini kwa awamu hii umekuwa ni “upepo wa kisuli suli’’si kwamba watu wanataka kutangaza majina yao hapana bali kila mmoja amesukumwa na moyo wake na kuona fahari kujitokeza ndani ya ccm kugombea nafasi.
Leave a comment