BENKI ya UBA nchini imeeleza kuwa, kwa sasa wanakwenda kwa wananchi baada ya mafanikio makubwa ya kufanya kazi na serikali. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Benki hiyo iliyofikisha miaka 10 tangu kuanzisha matawi yake nchini, imekuwa ikishirikiana na serikali katika kuwezesha kufanikisha miradi mikubwa nchini ikiwa ni pamoja na mradi wa sasa kufua umeme katika Mto Rufiji.
Usman Isiaka, Mkurugenzi Mkuu wa UBA nchini akizungumza na wanahabari amesema kuwa, tayari imefanya kazi kubwa na serikali na kwamba, kwa sasa inashirikiana katika ujenzi wa mradi wa kufua umeme katika Mto Rufiji.
Amesema kuwa, benki hiyo ilianza kufanya kazi hapa nchi kwa miaka 10 sasa na kwamba, ingawa wananchi wengine wamekuwa wakifaidika na benki hiyo, sasa wanakwenda chini kwa wananchi wengi zaidi.
Amefafanua kuwa, UBA tangu kuanzisha kwake, ina miaka 70 ambapo ina matawi mbalimbali ndani na nje ya Afrika.
“Lengo kuu ni kusaidia kiuchumi katika nchi za Afrika. Sisi kama benki tunafurahi kufanya kazi na serikali lakini wananchi ambao tayari wamekuwa wakipata huduma zetu,” ameeleza Isiaka.
Amesema, benki hiyo imeweka mkakati wa kuwa karibu zaidi ili kuendelea kutoa huduma zake zenye manufaa kwa wananchi hasa kwa kutumia mtandao.
Stella Matafu, Ofisa Mahusiano wa UBA amesema kuwa, mikakati iliyopo kwa sasa ni kuhakikisha Watanzania wanapata huduma nzuri za kibenki.
“Na hii ndio maana tumekuja na product (bidhaa) zetu nyingi za kidigitali ikiwemo Leo, Magic Bank ambazo zinaweza kumsaidia Mtanzania yeyote, aliyepo mahali popote ili aweze kupata huduma za kibenki,” amesema na kuongeza;
“Haihitaji kuwa na simu ya kisasa (smartphone), simu yoyote unaweza kufungua akaunti yake mahali popote ulipo. Hii itasaidia hata wale wa vijijini kupata huduma zetu.”
Leave a comment