TIMU ya Taifa wa Tunisia imejiweka pazuri kueleka katika Fainali za Mataifa Afrika (AFCON) baada ya kutoka sare katika mchezo wake wa ugenini dhidi ya Taifa Stars katika mchezo uliochezwa kwenye Uwanja wa Benjamini Mkata jijini Dar es Salaam. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Tunisia imefikisha pointi 10 na kujikita kileleni wa Kundi J baada ya kushinda michezo yake mitatu na kutoka sere ya bao 1-1 katika mechi ya leo, hivyo kuongeza matumaini ya kucheza fainali hizo zinazotarajiwa kuchezwa Januari mwakani nchini Cameroon.
Wakati Tunisia wakiwa kileleni mwa kundi hilo, nafasi ya pili inashikiliwa na Equatorial Guinea ikiwa na pointi sita baada ya kushinda mechi mbili na kupoteza michezo miwili, wakati Taifa Stars wapo katika nafasi ya tatu wakiwa na pointi zao nne walizopata kwa kushinda mechi moja, kutoka sare moja na kupoteza moja.
Nafasi ya mwisho kwenye kundi hilo inashikiliwa na timu ya Taifa ya Libya ambayo inapointi tatu baada ya kushuka uwanjani mara nne na kuambulia ushindi katika mchezo mmoja na kupoteza mechi tatu.
Kila timu katika kundi hilo zimebakika michezo miwili mkononi huku Tunisia ikiwa na matumaini makubwa kutokana na kuwaacha kwa tofauti na pointi nne timu inayomfuatia, wakati Taifa Stars wanatakiwa kushinda michezo yake yote miwili iliyobaki ili ifikishe pointi 11, lakini watategemea matokeo ya vinara wa kundi hilo na Equatorial Guinea katika mechi zao zilizobaki.
Mabao ya leo kwenye mchezo huo yalifungwa na Seifeddine Khaou kwa upande wa Tunisia kwenye dakika ya 10, kipindi cha kwanza, huku bao la kusawazisha la Taifa Stars likifungwa na Feisal Salum kwenye dakika ya 47 kipindi cha pili.
Timu ambazo tayari zimefanikiwa kufuzu kucheza fainali hizo kabla ya hatua ya makundi kumalizika ni Mali, Senegal na Algeria.
Leave a comment