MBUNGE wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu amesema shambulio la risasi alilofanyiwa akiwa mjini Dodoma lililenga kumnyamazisha dhidi ya kuikosoa serikali. Anaripoti Mwandishi wetu.. (endelea).
Lissu ambaye pia ni mnadhimu Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni ameyasema hayo leo akizungumza na wanahabari ikiwa ni mara ya kwanza tangu ashambuliwe na watu wasiofahamika nyumbani kwake Area D Septemba 7, mwaka jana.
Amesema kuwa dalili zinaonesha watu waliomshambulia kwa risasi mjini Dodoma mwaka jana walikuwa na uhusiano na serikali hivyo anailaumu serikali ya Rais John Magufuli kwa kuwakandamiza wapinzani.
Anaamini shambulio dhidi yake lililenga kumnyamazisha kutokana na uokosoaji wake wa mara kwa mara kwa serikali ambapo hadi kufikia sasa anaamini hakuna uchunguzi wa maana kuhusu kushambuliwa kwake mnamo 7 Septemba unaendelea.
“Tanzania imebadilika na kuwa taifa ambalo hakuna aliye salama. Mawakili wanaweza kurushiwa mabomu kwa kuwawakilisha wateja wao. Nchi ambayo afisi za mawakili zinaweza kuvamiwa, na mawakili kufungwa jela,” amesema Lissu.
Hata hivyo familia ya Lissu pamoja na Lissu mwenyewe inathibitisha kuwa tangu awali serikali haikuwa imekusudia kulipia gharama za Lissu kama ilivyothibitisha wakati mbunge huyo akiondolewa hospitali ya mkoa wa Dodoma kupelekwa nchini Kenya kwa matibabu ya kitaalamu zaidi na penye uhakika wa usalama wake.
Lissu amesema amepona na kwamba anashukuru Mungu na wote waliomtakia uponaji wa haraka.
Taarifa kutoka ndani ya familia ya mwanasiasa huyo na Lissu mwenyewe zinasema, mbunge huyo wa Singida Mashariki, anatarajiwa kuondoka mjini Nairobi, Jumamosi wiki hii (kesho).
Kwa mujibu wa taarifa hizo, Lissu anapelekwa moja ya nchi za Ulaya, jina na hospitali anayokwenda tunaihifadhi kwa sasa.
Leave a comment