Tuesday , 19 March 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Tundu Lissu afunguka mabadiliko ya CCM
Habari za SiasaTangulizi

Tundu Lissu afunguka mabadiliko ya CCM

Spread the love

From Tundu Lissu in Belgium

Kuhusu hoja ya Thadei Ole Mushi juu ya mabadiliko ya CCM

Mimi sio mwanachama wa CCM lakini kwa umuhimu wa hoja hii, na ukweli kwamba mabadiliko katika siasa za ndani za CCM yanatuathiri wote kwa njia mbali mbali, naomba kuichangia.

Kwanza, kuna mambo yanayohitaji uthibitisho wa Katiba na Kanuni za CCM. Je, kwa mfano, bado Baraza la Ushauri la waliokuwa viongozi wakuu wa CCM na Serikali???

Sina Katiba ya CCM hapa lakini nimewahi kusoma makala, nadhani ya Fatma Karume, ya mwaka jana kama sikosei, ambako alidai kwamba Baraza la Ushauri lilivunjwa wakati Kikwete akiwa Mwenyekiti wa CCM.

Tunahitaji uthibitisho wa hili ili tuweze kupima hoja ya ole Mushi juu ya majukumu au umuhimu wa chombo hicho.

Je, kuna ukweli gani kuhusu maneno yaliyojitokeza mwaka jana wakati wa Mkutano Mkuu wa CCM kwamba sasa, kwa mabadiliko ya Katiba ya CCM, Mwenyekiti wa CCM atakuwa automatically mgombea uRais wa CCM kwenye Uchaguzi Mkuu???

I hope umuhimu wa suala hili ni self-evident for any serious analysis of the current correlation of power within CCM.

Kama Mwenyekiti ni mgombea Urais bila kupingwa maana yake ni kwamba vikao vya maamuzi vya chama vitafanya kazi ya rubber stamp tu.

Eneo la tatu linalohitaji uthibitisho wa kikatiba linahusu composition ya Kamati Kuu ya sasa ya CCM. Ole Thadei ametupa composition ya Kamati Kuu ya CCM iliyopita, sio ya sasa.

Ninafahamu Kamati Kuu ya sasa ina wajumbe 24, ukilinganisha na 36+ wa iliyopita. Hawa wa sasa ni akina na, crucially, wanapatikanaje. Umuhimu wa hili nao should be self-evident kwenye analysis yoyote ya correlation of power within the party.

Baada ya utangulizi huu, sasa nitoe hoja yangu ya pili ambayo ni evolution ya CCM kama ‘chama-dola’ na sura yake ya sasa. Nadhani sitakosea nikisema kwamba angalau tangu mwaka ’64/’65, tumekuwa na ‘chama-dola’, yaani chama cha siasa ambacho kimeingiliana na vyombo vya dola kwa namna ambayo haviwezi kutenganishwa kirahisi, hata kwenye uchambuzi wa kitaaluma.

Chama-dola kilianza kwa wakati mmoja na kuzaliwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwaka ’64. Katiba ya kwanza ya Jamhuri ya Muungano ilitamka hivyo wazi kwa mara ya kwanza: Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar itakuwa nchi ya chama kimoja, i.e. TANU kwa Tanganyika na ASP kwa Zanzibar.

Mwaka huo huo, JWTZ ilianzishwa kufuatia maasi ya Tanganyika Rifles ya January ’64. Sehemu kubwa ya Jeshi jipya ilitokana na wanachama wa TANU Youth League. Baadaye kama inavyojulikana, vyombo vingine vyote vya dola, Utumishi wa umma na hata taasisi za kitaaluma viliingizwa kwa dragnet kubwa ya chama-dola.

Mageuzi ya kisiasa ya 92′ hayakubadili sana hulka ya CCM kama chama-dola. Makatazo ya uanachama wa vyama vya siasa katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano yaliyowahusu wanajeshi, watumishi wa umma na wa Mahakama yalificha uchama-dola wa CCM.

Haikuuondoa kama mifano mingi ya watumishi wa umma au wanajeshi au majaji wanaoacha utumishi wao halafu mara moja wakateuliwa kwenye nafasi kubwa za kichama, inavyothibitisha.

Aidha, kuna nafasi nyingine katika utumishi wa umma ambazo bado zinahusishwa moja kwa moja na CCM na zinadhihirisha uchama-dola wake. Kwa mfano, Wakuu wa Mikoa na Wilaya, ambao ni wenyeviti wa Kamati za Ulinzi na Usalama za maeneo yao na wana residual police powers, bado wanatakiwa na Katiba ya CCM kuwa wanachama na wajumbe wa vikao vyote vya maamuzi katika maeneo yao.

Sasa kipi kimebadilika kati ya CCM ya Kikwete na Makamba/Mkapa na Mangula na CCM ya sasa ya Magufuli??? Obviously, mabadiliko ni makubwa sana na yanakwenda mbali zaidi kuliko muonekano wa nje.

Kwanza, tangu Magufuli aingie madarakani na kuwa Mwenyekiti, ‘udola’ ndio umekuwa na nguvu zaidi kuliko ‘uchama’ wa CCM. Hili ni badiliko kubwa na la msingi.

Tangu miaka ya mwanzo ya chama-dola, ‘uchama’ wa CCM ulikuwa na nguvu na ulionekana wazi zaidi kuliko ‘udola’ wake. Vyombo vya dola vilikuwa ‘subsumed’ kwenye vyombo vya chama.

Maamuzi makubwa ya nchi yalifanywa kwanza na chama na baadae kutekelezwa na vyombo vya dola ambavyo na vyenyewe vilikuwa sehemu ya vyombo vya chama. CCM ya aina hiyo iliisha na Urais wa Ali Hassan Mwinyi, lakini mabaki yake yaliendelea hadi CCM ya Kikwete na Makamba.

CCM hiyo ilikuwa bado inafanya kazi ya siasa autonomously of vyombo vya mabavu vya dola; hata kama jambo hilo lilififia sana mpaka ikabidi Kikwete awaambie wanaCCM wafanye kazi ya siasa badala ya kutegemea kubebwa na vyombo vya dola.

CCM hiyo ilikuwa inaendeshewa Dodoma au Lumumba na Katibu Mkuu wake, whether Mangula wa Mkapa au Makamba/Mukama/Kinana wa Kikwete. CCM hiyo ilikuwa na uwakilishi mpana wa constituencies mbali mbali na ndio maana ya factionalism iliyokuwepo ndani yake.

CCM ya Magufuli ni tofauti kabisa. Hii ya sasa inaendeshewa Ikulu na Magufuli mwenyewe, sio Dodoma au Lumumba na Katibu Mkuu wake.

In fact, tukiweka ushabiki pembeni, ni sahihi kusema kwamba CCM ya sasa imekuwa haina Katibu Mkuu tangu Magufuli aingie madarakani.

Mnaweza kulinganisha tu tofauti kati ya Kinana wa Kikwete na Kinana wa Magufuli; au kati ya Nape Nnauye wa Kikwete na Humphrey Polepole wa Kikwete. Nape alikuwa Msemaji Mkuu wa CCM, sasa haijulikani kama Msemaji Mkuu ni Polepole wa Lumumba au Gerson Msigwa wa Ikulu.

Na haijulikani tena kama Ikulu ni Makao Makuu ya Rais, au nayo imegeuka kuwa Ofisi Ndogo ya CCM badala ya Lumumba au White House ya Dodoma. Ndio maana hata ole Thadei amechanganyikiwa.

Mabadiliko haya yamekwenda hata mikoani na wilayani. Huko CCM ya sasa inaendeshwa na Wakuu wa Mikoa na Wilaya, wakiwatumia au kusaidiwa na ma-RPC na ma-OCD.

Hii ndio maana halisi ya haya tunayoyaona ya akina Bashite, Gambo, Mnyeti na Malima na wengineo wengi. Kauli zao sio za bahati mbaya au za watu wasiojua wanachokifanya. Ni kauli zinazoonyesha uso halisi wa CCM ya sasa.

CCM hii haijishughulishi tena na kazi ya kawaida ya chama cha siasa: kushawishi wananchi kwa kutumia hoja za kisiasa. CCM ya Magufuli inakataza kazi ya kawaida ya chama cha siasa. Haina ushawishi wa wanasiasa, ina amri ya watawala.

Kwa sababu ni CCM ya amri, ndio maana vyombo vya mabavu vya dola sasa vimekuwa na umuhimu mkubwa katika siasa zetu. Badala ya hoja za kisiasa kujibiwa kwa hoja za kisiasa, sasa zinajibiwa kwa risasi za moto, mabomu na magereza.

Sasa majasusi wa polisi na Usalama wa Taifa wako kila mahali mitandaoni wakiwinda watu wanaofanya siasa za kawaida kabisa mitandaoni za kukosoa serikali au viongozi wake. Sasa tuna kosa jipya la jinai ambalo halipo kabisa kwenye Sheria zetu: ‘kumtukana Rais.’

Tumeingia kwenye giza nene katika siasa za nchi yetu kwa sababu ya mabadiliko haya katika siasa za CCM.

Kwa hiyo, suala muhimu sasa sio akina nani wako kwenye vikao vya juu vya CCM au kuna mikutano mingapi ya CC au NEC kwa mwaka. Suala muhimu zaidi ni vikao hivyo vina maana gani tena katika mazingira ambayo CCM ‘chama’ imefunikwa kabisa na CCM ‘dola.’

Tundulisu,
Ubelgiji,
29 Mei 2018.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

BiasharaHabari za Siasa

Zanzibar mbioni kuanza uchimbaji mafuta na gesi baharini

Spread the loveSERIKALI ya Zanzibar, imekamilisha mchakato wa uchimbaji wa mafuta na...

Habari za Siasa

Wizara ya afya yataja mafanikio 10 miaka mitatu Samia madarakani

Spread the loveWIZARA ya Afya imetaja mafanikio 10 iliyoyapata ndani ya miaka...

Habari za Siasa

Mbozi walilia kuwa manispaa, majimbo 3

Spread the loveHALMASHAURI ya wilaya ya Mbozi mkoani Songwe imeeleza dhamira yake...

Habari za Siasa

Wabunge waitaka TPDC kuongeza kasi ya kuunganisha wateja gesi asilia

Spread the love  KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini...

error: Content is protected !!