KLABU ya soka kutoka nchini DR Congo TP Mazembe inatarajia kuwasili nchini kesho kwa ajili ya mchezo wa Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Simba utakaochezwa Jumamosi ya tarehe 6, Aprili katika Uwanja wa Taifa, Jijini Dar es Salaam. Anaripoti Kelvin Mwaipungu … (endelea).
Afisa Habari wa Simba, Haji Manara amesema kuwa wapinzani wao wanatarajia kutua kesho majira ya saa saba mchana, tayari kwa mchezo wao wa raundi ya kwanza wa robo fainali ambapo kiingilio cha chini cha mchezo huo kitakuwa Sh. 4,000.
“Tumeweka viingilio rafiki sana kwa mashabiki wetu ili waweze kuja kushabikia timu yao uwanjani, ambapo kiingilio cha chini kitakuwa Sh. 4,000 na mpaka sasa tiketi zimeshaanza kuuzwa kwa mawakala wote,” Haji Manara
Msemaji huyo aliongezea kuwa tiketi za mchezo wao dhidi ya TP Mazembe za bei ya chini zitauzwa mwisho Ijumaa ambapo ikifika siku ya Jumamosi zitauzwa kwa Sh. 5,000 ili kuepusha msongamano siku ya mechi.
Simba imefanikiwa kufuzu robo fainali kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya kushika nafasi ya pili kwenye D baada ya kufanikiwa kupata ushindi kwenye mchezo wa mwisho dhidi ya AS Vita.
Mara ya mwisho timu hizo zilikutana mwaka 2011 katika hatua ya mtoano, ambapo mchezo wa kwanza uliochezwa Lubumbashi, Simba ilifungwa mabao 3-1, katika mchezo wa marudiano uliochezwa April 4, 2011 kwenye Uwanja wa Taifa, TP Mazembe iliibuka tena na ushindi wa mabao 3-2.
Leave a comment