HATIMAYE mwanaharakati na Ofisa wa Elimu wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Tito Magoti, Theodory Faustine, wamefunguliwa mashitaka matatu likiwemo utakatishaji fedha kiasi cha Sh. 17 milioni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Jeshi la Polisi limewafungulia kesi hiyo namba 137/2019 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam leo tarehe 24 Desemba 2019, baada ya kuwashikilia kwa siku nne.
Makosa mengine yanayowakabili ni kushirikiana na magenge ya uhalifu pamoja na uhalifu wa mitandaoni.
Mpaka wanafikishwa mahakamani, Tito na mwenzake tangu wakamatwe, haikuelezwa walipelekwa katika kituo gani cha polisi. Juhudi mbalimbali zilifanywa na familia yake pia LHRC bila mafanikio.
Wakili Anna Henga, Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC na familia ya Tito walitembelea vituo vyote vya polisi, lakini hawakufanikiwa kumwona ama kupata taarifa za wanaharakati hao.
Hata hivyo, tarehe 20 Desemba 2019, na SACP Lazaro Mambosasa, Kamanda wa Mkoa wa Dar es Salaam, aliuelezea umma kwamba, wanamshikilia mwanaharakati huyo.
Hakimu Mkazi Mkuu wa mahakama hiyo Janeth Mtega, ameahirisha kesi hiyo hadi tarehe 7 Januari, 2020 itakapotajwa.
Leave a comment