MTANDAO wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THDRC), umetuma wawakilishi wake kupeleka maombi ya dhamana kwa mwandishi Erick Kabendera. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Jeshi la Polisi leo limeeleza, linamshikilia mwandishi huyo wa habari za uchunguzi ndani na nje ya nchi. Limeeleza kuwa lina wasiwasi na uaria wake.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo tarehe 30 Julai 2019 na THDRC imeeleza, mawakili wake Jones Sendodo, Shilinde Swedy na Catherine Ringo wamepeleka maombi ya dhamana ya Kabendera mahakamani.
Taarifa ya mtandao huo inaeleza, maombi hayo ya dhamana Namba 14 ya mwaka 2019, yamepangwa mbele ya Hakimu Mwandamizi Rwizile na kusikilizwa Alhamisi ya tarehe 01 Agosti 2019.
“Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu umechukua hatua ya kupeleka maombi ya dhamana mahakamani, baada ya kufuatilia jana vituo vya polisi Oysterbay na Central na kuambiwa kwamba Erick hakuwepo katika moja ya vituo tajwa hapo juu,” inaeleza sehemu ya taarifa ya THRDC.
Kabendera alikamatwa na jeshi la polisi jana tarehe 29 Julai 2019 jioni. waliomkamata walivamia nyumbani kwake Mbweni na kuondoka naye.
“Tangu akamatwe, Erick hajapata nafasi ya kuwasiliana na wakili wake wala ndugu zake wa karibu,” imeeleza sehemu ya taarifa hiyo.
Leave a comment