MAWAKALA wa usambazaji mbolea kwa wakulima nchini wametakiwa kuweka mbolea zenye ujazo wa aina mbalimbali madukani ili wakulima wenye uwezo wowote wa kifedha na wenye mashamba madogo waweze kupata mbolea na kuboresha kilimo. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Mkaguzi wa mbolea kutoka Mamlaka ya udhibiti wa mbolea Tanzania (TFRA) Raymond Konga alisema hayo jana kwenye maonesho ya sikukuu za wakulima 88 kanda ya mashariki yanayofanyika katika viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere vilivyopo eneo la Tungi nje kidogo ya Manispaa ya Morogoro.
Konga alisema wakulima hasa wadogo wanapaswa kuondoa hofu ya kukosa mbolea ya kilogramu tano kufuatia viwanda na makampuni kuweka mbolea kwa ujazo mbalimbali kwenye maduka yao ya mauzo.
Alisema mawakala wengi wa mbolea wanapenda kuuza mbolea zenye ujazo kuanzia wa kilogramu 25 na 30 kutokana kupata wateja kwa wepesi tofauti na mifuko ya ujazo wa kilogramu tano ambayo haina na wateja wengi.
Hivyo aliwataka wakulima kutembelea maonesho ya sikukuu ya wakulima 88 kanda ya mashariki ili kujifunza teknolojia mbalimbali za kilimo ikiwemo matumizi sahihi ya mbolea na kuleta tija kwenye kilimo.
Awali Rehema Mbena mkulima wa mpunga kutoka Dakawa aliiomba TFRA kuingilia kati suala la upatikanaji wa mbolea za kilogramu tano kwenye maduka kutokana na ujazo huo kuwa adimu kwenye maduka ya pembejeo za kilimo.
“Kweli tunapata tabu wakulima wadogo, sababu hadi tujikusanye tukiwa watatu hivi…. na kununua mfuko mkubwa ndipo tugawane na kuendelea na kilimo, watuwekee mbolea za kilo tano madukani,” alisema Mbena.
Naye Afisa mauzo wa kampuni ya usambazaji pembejeo za Kilimo ETG inputs Ltd ya mjini Morogoro, Elisafi Mapunjo aliwataka wakulima wadogo mkoani hapa kuungana pamoja katika vikundi ili kuweza kuagiziwa mbolea ya kilogramu tano na kuepuka kuikosa kufuatia mbolea za aina mbalimbali kuwepo madukani katika ujazo wa kilo 25 na 50 pekee.
Mapunjo alisema, endapo wakulima watajikusanya na kufika 10 au zaidi wanaweza kufika kwenye ofisi au kwenye duka la kampuni hiyo iliyopo mjini Morogoro na Tanzania nzima kwa ujumla na kuweza kuagiziwa au kuelekezwa kwa wakala anayeuza mbolea kwenye mifuko ya kilo 5 ambayo kwa rejareja huuzwa kwa shilingi 5500.
Aidha Mapunjo alisema mbolea huwa zinaandaliwa katika ujazo mbalimbali kuanzia kilogram tano hadi 50 lakini wanashindwa kuiweka dukani kutokana na kukosa wateja wa haraka huku wakikosa ghala malumu la kuweka baada ya kutoka sokoni kufuatia ujazo huo kukaa mua mrefu dukani.
Hivyo aliwashauri wakulima kutumia mbolea kama inavyoelekezwa kwenye karatasi za matumizi au kutoka kwa wataalamu au maofisa kilimo wa maduka, wilaya au mikoa waliyopo.
“Wakulima wasikilize ushauri wa wataalamu na waache kilimo cha mazoea sababu mtu anakuja dukani anataka mbolea aina ya DAP… na DAP ni mbolea ya kupandia lakini ukimuuliza mazao yako yapo hatua gani anakwambia yapo hatua ya kutoa matunda… unaanza kumuelekeza lakini bado anakuwa mbishi jambo ambalo linatutia wasiwasi wa kufikia kinachokusudiwa kwenye maonesho haya,” alisema Mapunjo.
Leave a comment