SHIRIKISHO la mpira wa miguu Tanzania TFF limefungua dirisha la usajiri kwa klabu za Ligi Kuu, Ligi daraja la kwanza, Daraja la pili na Ligi Kuu ya wanawake kwa kipindi cha mwezi mmoja. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa kutoka ndani ya shirikisho hilo inaeleza kuwa, dirisha hilo limefunguliwa kuanzia tarehe 1 mpaka tarehe 31 Agosti, 2020 saa 5:59 usiku.
Kufunguliwa kwa dirisha hilo kutawapa fursa kwa klabu zinazoshiriki ligi hizo kuimarisha vikosi vyao kuelekea msimu mpya wa mashindano 2020/21 unaotarajia kuanza mwezi wa tisa.
Mpaka sasa klabu za Azam FC na Yanga zimeshaanza kufanya usajili kwa baadhi ya wachezaji ambapo mpaka sasa Azam FC imeshamsainisha kiungo mshambuliaji wa klabu ya Kagera Sugar Awesu Awesu huku klabu ya Yanga nayo ikiingia mkataba na kiungo Zawadi Mauya kutoka Kagera Sugar.
Simba pia imeshaanza usajili kwa kumsainisha beki kutoka Lipuli FC, David Kameta ambaye atavaa jezi nyekundu katika msimu ujao wa mwaka 2020/21.
TFF imeeleza kuwa hawata kuwa na muda wa nyongeza baada ya dirisha hilo kufungwa kama ilivyozoeleka hapo awali.
Leave a comment