SERIKALI ya Tanzania imeripoti kifo cha kwanza cha Mgonjwa wa Homa Kali ya Mapafu, inayosababishwa na Virusi vya Corona (COVID-19). Anaripoti Hamis Mguta…(endelea).
Taarifa ya kifo hicho imetolewa leo tarehe 31 Machi 2020 na Ummy Mwalimu, Waziri wa Afya na Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.
Taarifa ya Waziri Ummy inaeleza kuwa, kifo hicho kimetokea alfajiri ya leo katika Kituo cha Matibabu ya Wagonjwa wa COVID-19, kilichopo Mloganzila jijini Dar es Salaam.
Waziri Ummy amesema marehemu alikuwa mwanaume mwenye umri wa miaka 49, ambaye alikuwa anasumbuliwa na maradhi mengine.
“Ninasikitika kutangaza kifo cha kwanza cha mgonjwa wa COVID-19 hapa nchini kilichotokea alfajiri ya leo katika kituo cha matibabu ya wagonjwa wa COVID-19 kilichopo Mloganzila. Marehemu ni Mtanzania ambaye pia alikuwa anasumbuliwa na maradhi mengine,” inaeleza taarifa ya Waziri Ummy.
Aidha, Waziri Ummy amesema hadi kufikia leo idadi ya wagonjwa wa COVID-19 nchini ni 19, ambapo aliyepona ni mmoja na aliyefariki dunia mmoja.
Leave a comment