SERIKALI ya Afrika Kusini imesema inatambua mchango wa nchi ya Tanzania katika harakati za kuipatia uhuru nchi hiyo kupitia program ya urithi wa ukombozi wa Bara la Afrika, anaandika Dany Tibason.
Viongozi kutoka nchi hizo mbili wapo mjini Dodoma kwa ajili ya kuhudhuria mkutano wa siku tatu unaojadili urithi wa ukombozi wa Bara la Afrika.
Akizungumza na waandishi wa habari Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo nchini Tanzania, Elisante Gabriel amesema kuwa program hiyo imewakutanisha wataalamu, makatibu wakuu na mawaziri wa wizara mbalimbali zilizoshiriki katika vita vya ukombozi kutoka nchi hizo mbili kwa lengo la kuweka uelewano wa pamoja
“Lakini jambo lingine kubwa ni kwamba tunapenda kuweka historia vizuri ili hata vizazi vijavyo vitambue mchango wa Tanzania katika ukombozi wa Bara la Afrika ilikuwaje, na pia tufikie hatua ambapo kumbukumbu hizo ziwekwe kwenye mfumo wa kidigiti ambayo itatuzwa kwa muda mrefu zaidi” amesema Elisante.
Mkurugenzi mkuu wizara ya ujenzi nchini Afrika Kusini Mziwoke Dlabantu amesema kuwa nchi yao inatambua kazi kubwa ambayo imefanywa na Tanzania katika vita ya ukombozi wa nchi hiyo.
Washiriki wa mkutano huo watatembelea makaburi ya wapigania uhuru yaliyopo wilaya ya Kongwa iliyopo mkoani Dodoma.
Leave a comment