TAKWIMU zilizopo kwenye ripoti ya Benki ya Dunia (WB) na zile za serikali kuhusu kukua kwa uchumu, zinapingana. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
WB kwenye ripoti yake imeeleza kuwa, uchumi wa Tanzania kwa mwaka 2018 umekuwa kwa asilimia 5.2, wakati takwimu za serikali kupitia Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) zikionesha ukuaji wake ni wa asilimia 7 katika mwaka huo.
Ukuaji huo wa mwaka 2018 kwa mujibu wa NBS, ni ongezeko kutoka asimilia 6.8 ya ukuaji wa mwaka 2017.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo iliyozinduliwa tarehe 18 Julai 2019 jijini Dar es Salaam, imeonesha sababu kadhaa za WB kutofautina na takwimu za serikali, ikiwemo kasi ndogo ya ukusanyaji mapato kwa mujibu wa taarifa ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Udhibiti katika matumizi ya umma, pamoja na kupungua kwa thamani ya mauzo ya nje ya nchi.
Ripoti hiyo imeonesha kwamba, thamani ya mauzo ya nje ilipungua kwa asimilia 3.9, kufuatia kushuka kwa mauzo ya korosho ghafi nje ya nchi, huku ununuzi wa bidhaa za nje ukiongezeka kwa asilimia 7.8 hali iliyochochewa na ununuzi wa vifaa vya ujenzi wa miradi ya maendeleo.
Vile vile, ripoti hiyo imeonesha kwamba, kwa mwaka 2018 akiba ya fedha za kigeni ilipungua kutoka Dola za Marekani 5.8 Bilioni hadi 4.9 bilioni. Hata hivyo, ripoti hiyo imesema kiasi hicho cha fedha kina uwezo wa kuagiza bidhaa na huduma za nje kwa kipindi cha miezi minne.
Aidha, ripoti hiyo imeonesha kwamba, thamani ya Shilingi ya Tanzania iko imara kutokana na hatua ya Benki Kuu ya Tanzania (BOT), kudhibiti biashara ya ubadilishaji wa fedha za kigeni ikiwemo kufunga maduka ya fedha za kigeni yaliyokuwa yanaendesha shughuli zake kinyume na sheria.
Pia, ukuaji wa sekta ya uwekezaji ni wa kuridhisha, na hali ya deni la taifa limeendelea kubaki himilivu.
Leave a comment