MBUNGE wa Muleba Kaskazini,Charles Mwijage kwa mara ya kwanza ameuliza swali bungeni baada ya kuvuliwa wadhifa wa uwaziri wa viwanda na biashara na Rais John Magufuli Novemba 10 mwaka huu. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Leo tarehe 16 Novemba 2018 bungeni jijini Dodoma, Mwijage aliuliza swali kwa Wizara ya Nishati, akisema kuwa, kuna baadhi ya kata jimboni mwake ambazo zilitakiwa kuwashiwa umeme katika Mradi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) awamu ya pili, lakini awamu hiyo imeisha pasipo kata hizo kuwashiwa umeme.
“Mazingira ya Kigoma Kusini ni kama ya Muleba Kaskazini, katika mpango wa REA namba mbili mkandarasi alitandaza nyaya katika baadhi ya kata, wananchi hawakupata umeme, ningependa kujua lini watawashiwa umeme ili waweze kufaidika na umeme wa REA,” alihoji Mwijage.
Katika hatua nyingine, Mwijage alimshukuru Rais Magufuli kwa kumteua kuwa waziri awali, Makamu wa Rais, Samia Suluhu na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa pamoja na uongozi wa bunge kwa kumpa ushirikiano na kumuongoza katika majukumu yake.
“Nikushukuru wewe kwa niaba ya mheshimiwa Spika Job Ndugai kwa namna ambavyo tumekuwa tukishirikiana na kuniongoza katika kutekeleza majukumu yangu, pia ningependa kumshukuru rais, makamu wa rais na waziri mkuu kwa namna ambavyo walinipa majukumu na kuweza kunisimamia, mwisho nimshukuru Mungu,” amesema Mwijage.
Akijibu swali la Mwijage, Waziri wa Nishati, Dk. Medard Kalemani amesema kata hizo miradi yake ya umeme haijakamilika vizuri katika awamu ya pili, na kwamba miradi hiyo ya umeme itapelekwa katika mradi wa REA awamu ya tatu sehemu ya kwanza.
“Ni kweli maeneo ya Muleba Kaskazini kazi ya mkandarasi awamu ya pili haujakamilika vizuri, mradi huo umepelekwa awamu ya tatu sehemu ya kwanza, watapelekewa umeme katika raundi hii itakayofuata,”amesema Dk. Kalemani.
Leave a comment