WAKATI wabunge wa upinzani wakishinikiza marais waliopitisha mikataba mibovu kuhojiwa, Job Ndugai, Spika wa Bunge la Tanzania amewaibua Mawaziri wastaafu Edward Lowassa na Fredrick Sumaye, anaandika Hamisi Mguta.
Ndugai amesema kuwa wabunge wa Chadema wanaoshinikiza marais wastaafu wahojiwe wakumbuke kuwa chama hicho pia kina mawaziri wakuu wastaafu wawili ambao watahusika.
“Mabadiliko mnayoyataka yakipitishwa na viongozi mlionao wakikamatwa msije mkalalamika tena,” amesema Ndugai.
Mawaziri wastaafu waliopo Chadema ni Edward Lowassa aliyekuwa Waziri Mkuu wa Awamu ya Nne na Frederick Sumaye, Waziri Mkuu Mstaafu wa Awamu ya Tatu, ambao walihamia chama hicho wakitokea CCM mwishoni mwa mwaka 2015.
Katika mchango wake bungeni, Peter Lijualikali amesema, haiwezekani watendaji wa serikali wakapitisha mikataba mibovu ya madini bila ridhaa ya rais hivyo marais wastaafu wanatakiwa kuhojiwa.
“Haiwezekani Mzee wangu Chenge (Andrew) na Karamagi (Nazir) walipitisha mikataba hiyo bila Rais aliyekuwapo kufahamu. Kinga ya Rais kushtakiwa iondolewe ili wahojiwe,” amesema Lijualikali.
Hoja hiyo ya Lijualikali inafanana na ya John Heche (Chadema), Mbunge wa Tarime
Vijijini.
Leave a comment