Thursday , 28 March 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Sumaye akemea serikali kunyanyasa wapinzani
Habari za SiasaTangulizi

Sumaye akemea serikali kunyanyasa wapinzani

Frederick Sumaye, Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Pwani (katikati) akizungumza na waandishi wa habari hawapo pichani
Spread the love

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Kanda ya Pwani kimekemea serikali kwa matumizi mabaya ya sheria za nchi dhidi ya viongozi na wanachama wa vyama vya upinzani, anaandika Irene David.

Frederick Sumaye, Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Pwani, amewambia waandishi wa habari leo ofisini kwake Magomeni Dar es Salaam, kuwa manyanyaso wanayopata wapinzani nchini yanatokana na baadhi ya viongozi wa serikali kutumia vibaya madaraka waliyopewa.

Kwa sababu hiyo, amesema, nchi inatumbukia kwenye udikteta unaofichwa katika matumizi ya sheria kandamizi.

Sumaye amesema nchi yoyote inayofuata kanuni na misingi ya demokrasia ni lazima ifuate sheria, lakini isizitumie kunyanyasa watu. Amewataka viongozi wahakikishe wanafuata kanuni na taratibu husika katika kuhakikisha wanatenda haki.

“Inaonekana kwa wazi sasa kumekuwa na tabia ya baadhi ya wakuu wa wilaya kujichukulia sheria isivyopaswa. Vitendo hivyo ni vya kukemewa na sisi kama wapinzani. Hatutakaa kimya, lazima tuliseme ili wananchi waelewe hali inayoendelea nchini,” amesema.

Wiki iliyopita, Ally Hapi, Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, aliagiza jeshi la polisi kumkamata na kumweka ndani kwa saa 48 Halima Mdee, Mbunge wa Kawe (Chadema) baada ya mbunge huyo kutetea watoto wa kike wanaopata mimba shuleni, kinyume cha kauli ya Rais John Magufuli aliyesema watakaopata mimba hawataruhusiwa kuendelea na masomo.

Mdee, ambaye pia ni mwenyekiti wa Baraza la Wanawake wa Chdema (Bawacha), alisisitiza kuwa kauli ya rais inakiuka mikataba kadhaa ya kimataifa ambayo Tanzania imesaini ili kutetea na kulinda hali ya mtoto wa kike kupata elimu.

Alisisitiza kuwa wasichana wengi wanaopata mimba shuleni katika umri mdogo wanabakwa, na kwamba hiyo haipaswi kuwa sababu ya watoto hao kuharibikiwa ndoto za maisha yao kwa kukosa elimu.

Siku moja baadaye mkuu wa mkoa aliagiza mbunge huyo akamatwe kwa maelezo kuwa amemkashifu rais. Hata hivyo, badala ya saa 48 mbunge huyo alikaa mikononi mwa polisi kwa siku sita mfululizo, ambazo ni zaidi ya saa 72, kisha akapelekewa mahamakani.

Kabla ya tukio hilo, Kisare Makori, Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Jijiji Dar es Salaam, aliagiza kukamatwa kwa Boniface Jacob, Meya wa Ubungo, kwa kosa la kualika na kutembeza viongozi wa Chadema kukagua miradi ya maendeleo katika Manispaa ya Ubungo. Mkuu wa wilaya anadai huo ni ukiukaji wa maadili ya kazi.

Jacob alikaa ndani kwa saa 48 halafu akaachiwa. Hivi majuzi, mkuu wa wilaya ya Ukwerewe naye aliagiza polisi wamweke ndani mwenyekiti wa kijiji kwa saa 48 kwa sababu walitofautiana kauli.

Kwa mujibu wa Sumaye, haya ni matumizi mabaya ya sheria, na ni unyanyasaji wa raia, kwani hakuna sheria yoyote inayompa mkuu wowote wa wilaya mamlaka ya kukamata kiongozi yoyote anapokuwa anatumiza wajibu wake.

Alikemea pia tabia ya serikali kuminya uhuru wa habari kwa kutisha waandishi wa habari au wamiliki; akasema kama mambo haya yataachwa tu, nchi itelekea kubaya.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

Nani anasema kuna hasara ATCL?

Spread the loveRIPOTI za makusanyo na matumizi ya fedha katika Kampuni ya...

Habari za SiasaTangulizi

CAG: Wastaafu, wenza wao chanzo NHIF kufilisika

Spread the loveRIPOTI ya ukaguzi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu...

Habari za SiasaTangulizi

Vikundi hewa 851 vyalamba bilioni 2.6 mikopo ya halmashauri

Spread the loveVIKUNDI hewa vya wajasirimali wadogo 851 kutoka katika halmashauri 19...

Habari za SiasaTangulizi

Mashirika matano yapata hasara mabilioni ya fedha

Spread the loveMASHIRIKA matano ya Serikali yanayojiendesha kibiashara, yamepata hasara ya mabilioni...

error: Content is protected !!