JOSEPH Mbilinyi, Mbunge wa Mbeya Mjini amedai kuwa, kifo cha marehemu mama yake, Desderia Mbilinyi kilichotokea tarehe 26 Agosti, 2018 katika hospitali ya Taifa Muhimbili alikokuwa anapatiwa matibabu, kimesababishwa na yeye kufungwa gerezani bila hatia. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Mbilinyi maarufu kama Sugu ametoa madai hayo leo wakati akitoa wasifu wa marehemu mama yake katika ibada ya kuuaga mwili wa marehemu iliyofanyika kwenye Kanisa lililoko kwenye hospitali ya Muhimbili jijini Dar es Salaam.
Akieleza chanzo cha kifo hicho, Sugu amedai kuwa, mwezi Februari mwaka huu mama yake alipata tatizo la ugonjwa wa presha (BP) ikiwa ni wiki moja baada ya yeye kufungwa gerezani, na kwamba tatizo hilo lilimsababishia afya yake kuporomoka kwa kasi ikiwemo figo yake kufeli na kupelekea kufikwa na umauti.
“Mama alipata tatizo la BP alizidiwa ghafla mwaka huu mwezi Februari wiki moja baada ya mimi kufungwa gerezani, na mpaka mauti mama aliamini nilifungwa kwa kuonewa na kifungo kile kilimuumiza sana kupelekea afya yake kuporomoka kwa kasi,” amesema na kuongeza.
“Baadae presha ilipanda isivyokawaida na kusababisha figo kufeli, alianza kutibiwa hospitali ya rufaa Mbeya mwezi Februari na baada ya hali kuwa mbaya mwezi Julai alipewa rufaa ya kuja Muhimbili ambako aliendelea na matibabu mpaka alivyofariki Jumapili.”
Kuhusu wasifu wa marehemu Desderia Mbilinyi, Sugu amesema mama yake aliyezaliwa tarehe 25 Disemba, 1956 ameacha watoto watano.
Mwili wa marehemu Desderia Mbilinyi unasafirishwa kuelekea mkoani Mbeya kwa ajili ya mazishi ambapo misa takatifu ya kumuombea marehemu itafanyika kesho kuanzia saa nne asubuhi.
Leave a comment