JOB Ndugai, Spika wa Bunge na wabunge 48, leo usiku wanatarajia kwenda nchini Misri kuishangilia Timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ katika michuano ya Mataifa ya Afrika (AFCON). Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Mbali na timu hiyo ya Bunge, mchekeshaji Peter Molel ‘Pierre Konki Liquid’ ni miongoni mwa washangiliaji wanaotarajiwa kutua Misri kwenye safari hiyo.
Stars imepangwa kundi C pamoja na timu za Senegal, Algeria na Kenya ambapo Juni 23 mwaka huu, wanatarajiwa kushuka dimbani kucheza na Senegal.
Akizungumza bungeni leo tarehe 18 Juni 2019, mara baada ya kumalizika kwa kipindi cha maswali na majibu, Spika Ndugai amesema kuwa, anaondoka leo usiku kuelekea Misri kwa ajili ya kushuhudia fainali hizo.
“ ‘Trip (safari) hii imekuwa very fear (woga), tumejitahidi sana tutahakikisha wabunge wanapata Hotel ya Five Stars, wale wa Trip ya kwanza nitaiongoza mimi mwenyewe, na nitaondoka usiku wa leo. Kwa hiyo nitawapelekea salamu zenu.
“Tunachoomba kwenu ni kuendelea kuiombea timu yetu, na tumehakikisha Piere tunaenda nae ili kuhakikisha Taifa Stars inakuwa juu,” Amesema Spika Ndugai.
Amesema kuwa “Vijana wetu wa Taifa Stars tayari wapo kule Misri kwa ajili ya AFCON, tuliishasema kwamba, wabunge wajiandikishe kwa hiyo awamu ya kwanza tutakuwa na wabunge kama 48, ni idadi nzuri tumejitahidi sana kupunguza machungu kupitia ofisi yangu,”amesema.
Spika Ndugai amesema, kutokana na uzito wa michuano hiyo, ofisi yake imeamua kusaidia baadhi ya gharama za wabunge ambapo amedai uwepo wao nchini Misri, utawatia nguvu wachezaji wa Stars.
“Na tutawapa moyo sana vijana kwani mechi zile ni ngumu na ni hamasa kubwa kwa Watanzania, baada ya miaka 40 timu yetu inapata nafasi ile,” amesema.
Na kwamba, wameona Bunge lichukue jukumu la kuongoza hamasa ili vijana wanapocheza, waone na viongozi wao wamesafiri.
Leave a comment