HATUA ya Job Ndugai, Spika wa Bunge la Tanzania kumpa fursa ya kurejea bungeni Cecil Mwambe aliyejivua uanachama wa Chadema, sasa itamfikisha mahakamani. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Jumatano ya tarehe 6 Mei 2020, Spika Ndugai alilieleza Bunge, hafahamu kama Mwambe alijizulu ubunge.
Alitoa kauli hiyo baada ya kutumiwa barua na Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika, inayoelezea kuwa Mwambe siyo mbunge wa Chadema, kufuatia hatua yake ya kujiunga na Chama cha Mapinduzi (CCM).
“Mimi bado namtambua Mwambe kama mbunge halali wa Ndanda na namkaribisha bungeni wakati wowote anapotaka,” alisema Ndugai
uamuzi huo wa Spika Ndugai umelifanya Shirika la Uraia na Msaada wa Sheria (Cilao) kwa kushirikiana na wadau wengine wa sheria, kuanza mchakato wa kufungua kesi katika Mahakama Kuu dhidi ya kiongozi huyo wa Bunge kwa kile walichokiita ‘kuvunja sheria.’
Cilao limeeleza, sababu ya kumfikisha katika vyombo vya sheria Spika Ndugai ni kutokana na kumruhusu mtu asiye mbunge kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuhudhuria na kufanya shughuli za kibunge.
Odero Odero, Mkurugenzi wa Cilao mwishoni mwa wiki alisema, Bunge na vyama vya siasa vinaongozwa kwa mujibu wa Katiba na sheria zingine za nchi. Ibara ya 71 ya Katiba ya nchi inaeleza wazi kuhusu ukomo wa mtu kuwa mbunge.
Amesema, kwa mujibu wa ibara ya 71(1)(e) ya Katiba, ni wazi kuwa mbunge atapoteza nafasi yake ya ubunge ikiwa atapoteza uanachama wa chama chake kilichompatia udhamini wakati wa uchaguzi.
Kwa mujibu wa ibara hiyo, Odero amesema, Mwambe aliyetangaza kujivua uanachama wa Chadema tarehe ,,,, na kujiunga na CCM, hakupaswa kurudishwa bungeni bila kufanyika uchaguzi kwa mujibu wa Katiba.
“Kitendo cha Spika Ndugai cha tarehe 6 Mei 2020, kumruhusu Mwambe kurejea bungeni kama mbunge, ni ukiukwaji wa wazi wa sheria za nchi,” amesema.
Amesema, kwa mujibu wa Katiba ibara ya 26(1), inamtaka kila raia kusimamia na kutetea Katiba na sheria, hivyo shirika hilo na wadau wengine wanampeleka Spika Ndugai mahakamani.
Tarehe 15 Februari 2020, Mwambe alitangaza kujiuzulu nyadhifa zake na kujiunga na CCM katika mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika ofisi za CCM, Lumumba jijini Dar es Salaam.
Katika mkytano huo uliohudhuriwa na waandishi wa habari, Mwambe alipokewa na Humphrey Polepole, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM.
“Leo hii, tarehe 15 Februari 2020 kwa hiaria yangu, kwa kutumia haki yangu ya kikatiba, nimeamua mwenyewe kujiunga na Chama Cha Mapinduzi na nitagombea tena ubunge katika uchaguzi ujao, kupitia chama bora ambacho kinaheshimu demokrasia ya ndani.”
“Kina misingi imara ya uongozi, kinaheshimu wanachama na viongozi wake na kinajali maadili ya wanachama na viongozi wake na nitawaomba wananchi wangu wawe na subira na wanipokee endapo nitapewa ridhaa ya kufanya ivyo,” alisema Mwambe
Tarehe 22 Februari 2020, Dk Bashiru Ally akiwa kwenye ziara mkoani Mtwara alifanya mkutano Jimbo la Ndanda ambapo alitumia fursa hiyo kumkabidhi Mwambe kadi ya uanachama wa CCM.
Leave a comment