JOB Ndugai, Spika wa Bunge ameishauri Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kuangalia uwezekano wa kuongeza kilo zinazopimwa kwa abiria wanaosafiri na boti kwenda Zanzibar, kutoka kilo 20 za sasa. Anaripoti Danson Kaijage…(endelea).
Ndugai amedai kwamba, kilo hizo ni ndogo na kwamba, ipo haja ya kuliangalia upya suala hilo la mizigo kwa kuwa, kilo 20 linaweza kuwa na uzito sawa na begi la mwanafunzi.
Spika Ndugai ametoa kauli hiyo leo tarehe 10 Juni 2019, wakati wa kipindi cha maswali na majibu mara baada ya Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Elias Kwandikwa kumaliza kujibu swali.
Kwandikwa alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Maryam Msabaha (Chadema) ambapo amewataka wateja wote wanaotumia bandari kwenda Zanzibar kwa boti, wahakikishe mizigo yao inapimwa kabla ya kupakiwa ili wajue kama uzito wake unastahili kutozwa ushuru.
Katika swali lake, Msabaha amedai kwamba kumekuwa na kero kubwa kwa abiria wanaotumia bandari kwenda Zanzibar kwa boti ambapo hulipishwa ushuru wa bandari kwa mizigo hata boksi la kilo 10 au mchele kg 20 kwa malipo ya Sh.9750.
Leave a comment