SPIKA wa Bunge, Job Ndugai amepokea barua ya kujivua uanachama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na kujiuzulu nafasi ya ubunge kwa aliyekuwa Mbunge Jimbo la Monduli, Julius Kalanga Laizer. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea).
Taarifa hiyo ilitolewa jana tarehe 01 Agosti, 2018 na Kitengo cha Habari Elimu kwa Umma na Mawasiliano Ofisi ya Bunge.
“Kufuatia barua hiyo tayari Mheshimiwa Spika amemuandikia Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Mheshimiwa Jaji Semistocles Kaijage kumfahamisha kuwa Jimbo la Monduli lililoko Mkoani Arusha liko wazi tangu sasa,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.
Mheshimiwa Spika ameandika barua hiyo kwa mujibu wa kifungu 37(3) cha Sheria ya Taifa ya Chaguzi (Sura ya 343, ya mwaka 2015)kinachoelekeza kwamba, pale ambapo Mbunge, atajiuzulu, atakufa au sababu nyingine yeyote tofauti na zilizoainishwa katika kifungu cha 113, Spika atamjulisha Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi na kutangaza kwenye Gazeti la Serikali kwamba kiti hicho cha Ubunge kiko wazi.
Taarifa hiyo ilieleza kuwa, kufuatia barua hiyo Tume ya Taifa ya Uchaguzi, inaweza kuendelea na mchakato wa kumpata Mbunge wa kujaza nafasi hiyo iliyowazi ya Jimbo la Monduli.
Leave a comment