Saturday , 20 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Spika Ndugai, ang’ang’aniwa mithili ya mpira wa kona
Habari za Siasa

Spika Ndugai, ang’ang’aniwa mithili ya mpira wa kona

Spread the love

RAIS wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Fatma Karume na Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT-Wazalendo), wamekosoa kauli ya Spika wa Bunge, Job Ndugai, kutaka Prof. Mussa Assad, kuhojiwa mbele ya Bunge. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).

Zitto na Fatma Karume, wametoa kauli hiyo, muda mfupi baada ya Spika Ndugai kuagiza mdhibiti na mkaguzi huyo mkuu wa serikali (CAG), kufika mbele ya Kamati ya Haki, Kinga, Maadili na Madaraka ya Bunge, ili kuhojiwa juu ya madai yake kuwa Bunge limeshindwa kusimamia serikali na dhaifu.

Akiandika katika ukurasa wake wa Twitter, kiongozi huyo wa mawakili nchini amesema, “Ndugai ameingia katika mamlaka isiyomuhusu.”

Amesema, kanuni za Bunge zilizopo sasa, hazimpi madaraka Spika au Kamati ya Maadili kumuhoji CAG kwa madai ya kudhalilisha Bunge.

Anasema, “…kanuni hizi, zinawahusu wabunge pekee. Hawa ndio wanaoweza kuhojiwa na kupewa adhabu kwa kukiuka kanuni za Bunge chini ya Kanuni ya 72,73 na 74.”

Fatma ambaye ni mjukuu wa rais wa kwanza wa Zanzibar, Abeid Amani Karume na mtoto wa rais mstaafu, Amani Karume anahoji: “Kudhalilisha Bunge ni nini haswa? Hakuna sheria hiyo! Tusitumie madaraka yetu, kudhalilisha wengine.”

Anasema, kanuni ya 71 ya Kanuni za Bunge za mwaka 2016, zinampa haki mwananchi ya kujitetea na kujisafisha dhidi ya kauli zinazotolewa bungeni na kwamba ili kufikia huko, kuna taratibu ya kufuata.

Binafsi, Fatma anasema, “mpaka sasa sijaona mamlaa ya Bunge ya kumkataza raia au CAG kuongea. Naendelea kutafuta.”

Naye Zitto ameandika katika ukurasa wake kama huo wa Twitter, kuwa Spika Ndugai hakustahili kutoa kauli hiyo.

Amesema, Spika Ndugai ametoa kauli ya dharau kwa Prof. Assad na ofisi mzima yake. Ni dharau kwa taasisi za uwajibikaji, na kwamba hakuna mamlaka yeyote nchini inayoweza kumhoji CAG isipokuwa tu kwa mashtaka mahakamani.

Amesema, “Spika wa Bunge hana mamlaka ya kisheria yaa kumwita CAG mbele ya Kamati ya Maadili. Wito wake kwa Prof. Assad, ni dharau kubwa kwa taasisi za uwajibikaji, katika nchi yetu na ni dalili za kulewa madaraka.”

Zitto ambaye ni kiongozi mkuu wa chama cha ACT- Wazalendo, amewataka wananchi, popote waliko, kutokubali CAG ambaye ni mlinzi wa fedha za umma kudhalilishwa.

“Tunajua hizi ni mbinu za kumkatisha tamaa Prof. Assad katika utendaji wake. Tusikubali adhalilishwe kwa kuhojiwa na Kamati ya Maadili ya Bunge. Hilo likitokea ni sawa na kuua kabisa uhuru wake. Kila mtu afikirie njia bora na sahihi ya kumzuia Spika Ndugai kufanya dhambi hii mbaya kabisa,….” anasisitiza.

Akizungumza na waandishi wa habari, mjini Dodoma, Spika Ndugai alimtaka Prof. Assad, kufika mbele ya kamati hiyo, tarehe 21 Januari 2019, ili kujibu “tuhuma za kudhalilisha Bunge.”

Alidai kuwa amefikia maamuzi hayo, baada ya kujiridhisha kuwa mkaguzi huyo wa fedha za umma amelidhalilisha Bunge na kwamba yeye kama kiongozi wa mhimili huo, hayuko tayari Bunge linadhihakiwa.

Amesema, “…namtaka Prof. Assad, kufika mbele ya Kamati ya Haki, Kinga, Maadili na Madaraka ya Bunge, kwa hiari yake, tarehe 21 Januari mwaka huu. Akishindwa, nitaagiza akamatwe na kuletwa mbele ya kamati kwa pingu.”

Aidha, spika huyo ameagiza mbunge wa Chadema katika jimbo la Kawe, Halima James Mdee, kufika mbele ya kamati hiyo, tarehe 22 Januari mwaka huu.

Ndugai anasema, Mdee ameitwa mbele ya Kamati ya Bunge, kutokana na matamshi yake ya kuuuga mkono kauli ya Prof. Assad.

Katika hatua nyingine, wanasiasa kadhaa na wanaharakati, wamepinga hatua ya Ndugai kumuita CAG mbele ya Kamati ya Bunge ili kuhojiwa.

Akizungumza na mwandishi wa habari wa MwanaHALISI Online, mbunge wa Tarime Vijijini (Chadema), John Heche amesema, “Bunge ni chombo cha wananchi. Wabunge wanalipwa mahashara na posho kwa kodi za Watanzania tena wengine wakiwa hawana uwezo wa kula hata milo miwili. Ni vema kikakubali kukosolewa.”

Amesema, “wananchi wana haki ya kuhoji na kukosoa uendeshaji na utendaji wa bunge lao. Achilia mbali CAG ambae sheria inamlinda.”

Naye Amani Mtei, katika andishi lake alilolisambaza kupitia mitandao kadhaa ya kijamii anasema, “kumhoji CAG kwa kusema bunge ni dhaifu, ni kudhiirisha udhaifu wenyewe.”

Anasema, “njia bora ilikuwa kuliongezea Bunge makali ya kuisimamia serekali ili kuonyesha kuwa siyo dhaifu kwa vitendo.

Kwa upande wake, Kashasira Alisted Malema, ameeleza katika ukurasa wake wa Twitter, “mwambie Spika asome katiba hasa Ibara ya 144, itamsaidia kujua namna ya kudili na CAG; siyo kutafuta kikiiii.”

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

BiasharaHabari za Siasa

Mavunde aagiza Perseus kuharakisha fidia Sengerema

Spread the loveWaziri wa Madini, Anthony Mavunde ameipongeza Kampuni ya Perseus kwa...

Habari za Siasa

Kigogo Chadema awanyooshea vidole vigogo serikalini kuhusu ripoti ya CAG

Spread the love  MWANACHAMA wa Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Boniface Jacob, amedai...

Habari za Siasa

Wabunge waikalia kooni TAKUKURU Bungeni

Spread the love  BAADHI ya wabunge wamelia na changamoto za utendaji wa...

Habari za SiasaTangulizi

Mpina ataka Waziri Majaliwa ajiuzulu, akosoa teuzi za mawaziri

Spread the love  MBUNGE wa Kisesa, Luhaga Mpina, amemtaka Waziri Mkuu, Kassim...

error: Content is protected !!