MKUU wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Simon Sirro, amefanya mabadiliko ya makamanda wa polisi katika maeneo kadhaa, anaandika Catherine Kayombo.
Miongoni mwa waliobadilishwa vituo vya kazi ni Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Susan Kaganda, aliyekuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, ambaye amepelekwa kuwa Mkuu wa Kitengo cha Mafao na Fidia, makao makuu ya polisi.
Nafasi ya Kaganda imechukuliwa na Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), Murilo Jumanne Murilo, aliyekuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga.
Aliyeteuliwa kuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ni Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Simon Haule, aliyekuwa afisa mnadhimu wa Polisi Mkoa wa Mara.
Kwa mujibu wa taarifa ya Jeshi la Polisi kwa vyombo vya habari, iliyosainiwa leo na Msemaji wa Polisi, Barnabas Mwakalukwa, mabadiliko hayo ni ya kawaida ndani ya jeshi hilo.
Leave a comment