SINEMA ya kukamatwa wabunge wa upinzani na kuwasafirisha kwa ndege wakiwa chini ya ulinzi mkali wa Polisi imejirudia leo baada ya Mbunge wa Ubungo, Saed Kubenea (Chadema), kusafirishwa alfajiri kwenda mjini akitokea jijini Dar es Salaam, anaandika Mwandishi wetu.
Kubenea amefikishwa mjini Dodoma baada ya jana kukamatwa akiwa hospitali jijini Dar es Salaam alipoenda kupata matibabu na kulazwa kituo cha Polisi cha Oysterbay kabla ya leo alfajiri kupandishwa ndege kwenda kutoa maelezo mbele ya Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Bunge.
Mbunge huyo amekamatwa kwa amri ya Spika Job Ndugai ambaye wiki iliyopita aliviagiza vyombo vya dola kumsaka popote alipo Mbunge huyo na kumkamata.
Kosa la kukamatwa Kubenea lilitokana na kutofautina na Spika kuhusu idadi halisi ya risasi alizopigwa Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu mjini Dodoma .
Mbunge huyo alisema Lissu alipigwa risasi 38, huku Spika akisema idadi ilikuwa 32 na baada ya kupishana huko, aliagiza Kubenea akamatwe ili akatoe ushahidi kwa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Bunge ambayo pia inaendelea kuchunguza tukio hilo.
Kukamtwa kwa Kubenea kunaonekana kama Sinema ambayo imezoelekwa kwa kuwa siyo mara ya kwanza wabunge wa upinzani kusafirishwa kwa ndege chini ya ulinzi mkali wa polisi.
Miongoni waliowahi kusafirishwa kwa ndege ni pamoja na Ester Bulaya ambaye ni Mbunge wa Bunda (Chadema), kwa amri ya Spika pamoja na Freeman Mbowe aliyesafirishwa kwa ndege pia kwenda jijini Arusha kuhudhuria kwenye kesi.
Taarifa zinasema Kubenea amewasili leo mjini Dodoma saa moja asubuhi na kwamba badio afya yake siyo nzuri na hivyo hajui kama anaweza kusimama na kuhojiwa na kamati hiyo.
Aidha, taarifa hiyo imesema Kubenea bado ana maumivu makali sana na kwamba hajaambiwa atahojiwa wapi na saa ngapi.
Kubenea amemshukuru Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Mandeleo ya Makazi, Angelina Mabula ambaye amesema amesaidia katika hali yake ya ugonjwa mpaka kufika Dodoma baada ya kukutana naye kwenye ndege leo asubuhi.
Leave a comment