JESHI la Muungano wa Kiuchumi wan chi za Magharibi mwa Afrika (ECOWAS) limezinasa silaha mbalimbali za kivita nyumbani kwa Yahya Jammeh Rais aliyelazimishwa kung’oka madarakani na kutimkia uhamishoni nchini, Guinea ya Ikweta, anaandika Wolfram Mwalongo.
Gazeti la Freedom la Gambia, limeripoti kuwa Jeshi la Ecowas likishirikiana na Jeshi la nchi hiyo limefanikiwa kuzikamata silaha za kivita zilizofichwa ndani ya makazi ya Jammeh yaliyopo Kanilai, Mashariki mwa Banjul ambao ni mji mkuu wan chi hiyo.
Itaumbukwa kuwa mahali hapo ndipo Jammeh alizaliwa na hata baada ya kuridhia kung’oka madarakani aliomba aruhusiwe kuishi katika makazi hayo lakini ombi hilo lilikataliwa.
Jeshi la Ecowas lipo nchini Gambia tangu kuzuka kwa hofu ya machafuko mapema Disemba mwaka jana huku Adama Barrow Rais wa sasa akionekna kuendelea kulipigia chapuo liendelee kubaki katika taifa hilo angalau kwa kipindi cha miezi sita hadi hali ya usalama itakapotengamaa.
Rais Barrow amewasili Gambia wiki mbili zilizopita kutoka uhamishoni nchini Senegal, lakini bado hajaingia Ikulu kutokana na uchunguzi unaoendelea kufuatia taarifa kuwa baadhi ya vyumba vya Ikulu viliwekwa sumu na Jammeh ili kumdhuru yeyote atakayeingia Ikulu ya nchi hiyo.
François, Jenerali anayesimamia kikosi cha Ecowas nchini Gambia amesema bado wanazishikilia silaha zilizokamatwa ingawa hakutaja idadi kamili ya silaha hizo. Amewahakikishia raia wa Gambia kuwepo kwa ulinzi wa kutosha na kwamba hakuna chochote kibaya kinaweza kutokea.
“Silaha zote na vifaa vya kijeshi kwa sasa viko mikononi mwa Ecowas. Hakuna kitu kibaya kitakachotokea huko Kanilai. Hali ya usalama imedhibitiwa na vikosi vya Jeshi la Gambia vinashirikiana vizuri ECOWAS,”ameserma François.
Leave a comment