CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimewaita wabunge wake 19 wa viti maalumu kujieleza kwa nini walikiuka maagizo ya chama hicho kutokubali uteuzi wa nafasi hizo. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Wabunge hao, wametakiwa kufika Ijumaa tarehe 27 Novemba 2020 saa 2:00 Makao Makuu ya Chadema, Kinondoni jijini Dar es Salaam ili kujieleza mbele ya kamati kuu ya kilichotokea kwenda kuapa bungeni.
Wabunge hao, wakiongozwa na Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake la Chadema (Bawacha), Halima Mdee waliapishwa jana Jumanne viwanja vya Bunge jijini Dodoma na Spika Job Ndugai.
Mbali na Mdee aliyeapishwa, wengine ni, Grace Tendeka, ambaye ni Katibu Mkuu wa Bawacha, Hawa Mwaifunga, Makamu Mwenyekiti wa Bawacha na Jesca Kishoa, Naibu Katibu Mkuu wa Bawacha na Agnesta Lambat, katibu mwenzi wa Bawacha.
Soma zaidi:-
Wengine ni; Esther Matiko, Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Serengeti ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu, Nusrat Hanje, Katibu Mkuu wa Baraza la Vijana wa Chadema (Bavicha).
Pia, Mjumbe wa Kamati Kuu, Ester Matiko, Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Mtwara, Tunza Malapo na Cecilia Pareso.
Wabunge wengine ni; Asia Mwadin Mohamed, Felister Njau, Naghenjwa Kaboyoka, Sophia Mwakagenda, Kunti Majala, Stella Siyao, Salome Makamba na Anatropia Theonest, Conchesta Lwamlaza.
Leo Jumatano, tarehe 25 Novemba 2020, akizungumza na waandishi wa habari makao makuu ya Chadema Kinondoni jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa chama hicho, John Mnyika amesema, wameisha kikao cha kamati kuu cha dharula.
Amesema, kikao hicho, kitaongozwa na Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na watawaandikia barua ya kuwaita mbele ya kamati kujieleza juu ya usaliti walioufanya.
“Chama inabidi kichukue hatua. Chama hiki kinaendeshwa kwa mujibu wa katiba, kanuni na maadili na itifaki ya chama kwa kuwa tunaendesha kwa mujibu wa katiba, tutawaita wahusika wote ,” amesema Mnyika.
“Katiba imetoa mfumo wa kushughulikia masuala hayo, inabidi hatua zisichukuliwe bila wahusika kuitwa kujieleza. Kwa kuwa hili jambo ni la dharura nawatangazia chama kitatumia utaratibu wa dharula kushughulika na jambo hili,” amesema Mnyika.
“Tumeitisha kikao maalumu cha Kamati Kuu tarehe 27 jijini Dar es Salaam pamoja na kuawandikia barua wahusika ili kisitokee kisingizo cha yoyote kwamba hakuitwa kujieleza.”
“Naomba kutangaza wito kwa wanachama wetu 19 walioshiriki kwenda kula kipao jana kufika makao makuu ya chama bila kukosa saa 2:00 asubuhi,” amesema Mnyika.
Mnyika amesema, kauli iliyotolewa na Mdee kwamba wana Baraka za chama na Mwenyekiti, Mbowe hazina ukweli “Mbowe ataongoza kamati kuu na itawasikiliza wahusika. Kati ya walioapishwa kuna wajumbe wa kamati kuu wanafahamu fika uteuzi haukufanyika na wanajua wameshiriki biashara haramu.”
Katibu mkuu huyo amesema “Chama hiki kitaendelea na kitapita salama. Kitaendelea kujipanga kwenda kushika dola. Chadema kimekuwa kikiwaita viongozi wakubwa wanaokiuka taratibu, kuhojiwa na kuchukuliwa hatua na bado kikavuka salama na kuwa tegemeo la Watanzania.”
Leave a comment