KAMATI Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM), imetoa siku saba kwa Kamati Ndogo ya Udhibiti na Nidhamu, kukamilisha taarifa ya mahojiano ya Bernard Membe, Waziri wa Mambo ya Nje Mstaafu na Makatibu Wakuu Wastaafu wa chama hicho, Mzee Yusuph Makamba na Abdulrahman Kinana. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Kwa mujibu wa Taarifa iliyotolewa na Humphrey Polepole, Katibu wa Itikadi na Uenezi (CCM) , imesema Kamati Kuu iliyoketi leo tarehe 12 Februari 2020 jijini Dar es Salaam, chini ya Rais John Magufuli, imeitaka kamati hiyo kuwasilisha taarifa hiyo kwenye vikao husika.
Aidha, taarifa ya Polepole inaeleza kwamba, Kamati Kuu ya CCM imepokea taarifa ya awali kutoka kwa kamati hiyo ndogo ya udhibiti na nidhamu.
“Kamati Kuu imepokea taarifa ya awali kutoka kwa Kamati ya Usalama na Maadili juu ya utekelezaji wa azimio la Halmashauri Kuu ya Taifa katika kikao chake cha mwezi Desemba jijini Mwanza kuhusu kuwaita na kuwahoji wanachama watatu, Mzee Makamba, Kinana na Membe ambao wote wameshafika mbele ya Kamati Mdogo ya Udhibiti na Nidhamu inayoongozwa na Mzee Phillip Mangula,” inaeleza taarifa ya Polepole na kuongeza:
“Kamati Kuu imetoa siku saba kwa Kamati Ndogo ya Udhibiti na Nidhamu, kukamilisha taarifa inayowahusu wanachama hawa watatu na kuwasilisha katika vikao husika.”
Agizo hilo la Kamati Kuu ya CCM, limetolewa siku kadhaa baada ya wanachama hao wa CCM kuhojiwa na kamati hiyo katika nyakati tofauti, ambapo Membe alihojiwa jijini Dodoma wakati Mzee Makamba na Kinana wakihojiwa jijini Dar es Salaam.
Wanachama hao wa CCM wanatuhuma kwa kukiuka maadili ya chama hicho kutokana na sababu mbalimbali, ikiwemo madai ya kutoa kauli zinazodhalilisha viongozi wa serikali.
Leave a comment