SHIRIKA la Posta Tanzania, limezindua nembo mpya ya shirika hilo baada ya ile ya zamani kukaa zaidi ya miaka 24 hadi kufika leo, anaandika Nasra Abdallah.
Hafla hiyo pia iliendana na uzinduzi wa mabasi yatakayotumika kusafirishia abiria na vifurushi kama njia mojawapo ya kuifanya kazi hiyo kwa usalama zaidi.
Akizungumza katika uzinduzi huo ulifanywa leo jijini Dar es Salaam, Naibu Waziri Wa wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Elias Kwandikwa amesema nembo hiyo ni moja ya utekelezaji wa mageuzi yanayofanywa kwa sasa na shirika hilo.
Kwandikwa amesema mageuzi hayo ni pamoja na uanzishwaji wa kampuni tanzu nne sambamba na mabadiliko ya muundo na mifumo ya kiutendaji itakayosaidia katika kusimamia na kuendesha miradi itakayoanzishwa.
“Ni hivi karibuni mlizindua huduma ya ya ‘Posta Mlangoni’, hicho pekee ni kielelezo sahihi cha jitihada hizi na matarajio yangu kuwa huduma mpya zitasimamiwa kikamilifu ili ziweze kufikia malengo yaliyokusudiwa,” amesema Waziri huyo.
Kuhusu mabasi matatu yaliyozinduliwa, Postamasta Mkuu, Hassan Mwang’ombe amesema wameyapata kutoka Umoja wa Posta Duniani baada ya kuridhishwa na utendaji kazi wa shirika hilo ambayo thamani yake yote ikiwemo Lori la tani 10 ni sh. 757 milioni.
Mwang’ombe amesema kwa kuanzia mabasi hayo yatakuwa yakibeba barua, vifurushi na abiria katika baadhi ya njia zenye shida ya usafiri ikiwemo Makambako (Njombe) na Masasi (Mtwara).
“Pamoja na kwamba lengo kuu la kupeleka mabasi hayo maeneo hayo ni kusafirisha barua na vifurushi ili kuongeza kasi ya usalama, ni wazi kuwa gharama za uendeshaji zitafidiwa na tozo ya nauli watakayotozwa abiria watakaotumia mabasi hayo na kuyafanya yaweze kumudu gharama za uendeshaji,” amesema Postamasta huyo.
Awali Mwenyekiti wa Bodi wa Shirika hilo, Kanali Mstaafu Haroun Kondo, amesema mpaka walipofikia sasa haikuwa kazi rahisi na imetokana na ushirikiano mkubwa uliopo Kati ya wafanyakazi, menejimenti na Bodi.
Kanali Kondo amesema pamoja na mambo mengine shirika litaendelea kuboresha matawi take ya ofisi za posta zilizoko mikoani na wilayani ili ziweze kutoa huduma bora zaidi na kuchangia uchumi na jamii kwa ujumla.
Leave a comment